1/18/13

NADHARIA YA CENTRE – PERIPHERY NA GESI YA MTWARA


Picha nimetoa kwa Issa Michuzi

NADHARIA YA CENTRE – PERIPHERY NA GESI YA MTWARA

Utangulizi

Kuna nadharia anuwai za maendeleo, kwa kadri nilivyofundishwa na walimu wangu wa somo la maendeleo (Development Studies). Na kila nadharia ina uzuri wake na ubaya wake, lakini kinachoamua uzuri ama ubaya wa nadharia hizo ni UTEKELEZAJI. Iwapo utekelezaji wa nadharia husika ni mbovu, hata nadharia iwe nzuri kiasi gani lazima kutakuwa na mapungufu.  

Nadharia ya Center Periphery /Core-Periphery

Nadharia hii imekuwa ikitumika kwa muda mrefu kuelezea uwiano hasi wa maendeleo kati ya nchi zilizoendelea na zile zilizo nyuma kimaendeleo. Mfumo huo umetumika sana na wanazuoni kama Samir Amin, A.G. Frank na Emmanuel Walerstine katika maandiko yao kwenye kuelezea maendeleo kwa mtazamo huo. Walijikita zaidi kwenye nadharia za za maendeleo za wafikiari wakuu kama Karl Marx. Kwa ufupi ni kwamba nadharia hii inaelezea mfumo usio sawa unaotokana na ubepari, katika mgawanyo wa rasilimali na maendeleo ya dunia. Nadharia hii inaongelea maendeleo ya “NCHI” na nchi, mie nimeamua kuishusha na kuihusianisha na “MKOA” na mkoa.

Nina uhakika kwamba serikali imeamua kutumia nadharia ya (Center-Periphery), kwa hili la Mtwara. Tuna uhakika 100% kuwa gesi ipo Mtwara, na sehemu ya gesi hiyo ndiyo inayotumika Ubungo kwenye uzalishaji wa umeme. Sasa, iwapo tujenge mfuo wa umeme Mtwara na kuusafirisha kwa nguzo za msongo mkubwa kwenda sehemu nyingine za Tanzania ni uamuzi mmoja, na iwapo tusafirishe gesi kwa bomba na kuipeleka Dar kisha tujenge mfuo wa umeme hapo ni uamuzi mwingine. Maamuzi ya mfumo upi utumike yapo mikononi mwa tuliowapa madaraka, wakisaidiana na wataalamu wa mipango.

Nadharia ya (Centre-Periphery) ina mtazamo wa kwamba kuna baadhi ya maeneo (iwe ni mkoa, majimbo, wilaya ama kata), ambayo kazi yake ni kuzalisha malighafi na kupokea bidhaa zitonakazo na malighafi hizo. Haiwezekani kuweka viwanda vya kuchakata malighafi hizo maeneo hayo, kwa sababu hayo maeneo "YATAFAIDI". Nadharia hiyo pia inaelezea kwamba maeneo mengine «yamegeuzwa» ni ya kuchakata kila malighafi, hata kama malighafi hiyo haitoki hapo. Haya ni maeneo ya viwanda tu, hata kama gharama za kusafirisha malighafi za viwanda hivyo ni ghali sana, kwa hiyo ajira zote zitokanazo na viwanda lazima "ZIWE HAPO TU". Kwa mujibu wa nadharia hii hii, maeneo mengine ni kwa ajili ya kuzalisha wasomi tu, ili kusaidia kuchakata na kuuza bidhaa na huduma zitokanazo na bidhaa zilizochakatwa. Sijajua Mtwara iko sehemu ipi hapo katika hiyo nadharia ya CENTER-PERIPHERY, kiasi kwamba serikali haitaki kujenga mifuo ya umeme na kusafisha gesi Mtwara wala kujenga barabara za kufika maeneo hayo.


Picha nimetoa kwa Issa Michuzi

Kwa nini Mtwara wanalalamika?

Viwanda vingi vipo Dar Es Salaam, japo Dar Es Salaam haizalishi malighafi zinazosindikwa na kuchakatwa katika viwanda hivyo. Kiwanda cha Sigara kipo Dar, pamoja na kwamba tumbaku inatoka Rukwa, Mbeya, Tabora na kwingineko. Viwanda vya kuzalisha juisi za matunda vipo Dar, japo matunda yanatoka mikoa anuwai kama vile Tanga, Iringa, Morogoro, Mbeya na Pwani. Viwanda vya mafuta ya kula vipo Dar, ilhali chikichi na alizeti zinazalishwa nje ya Dar. Uwiano huu usio sawa ndio unaozua malalamiko kwenye jamii, kiasi cha kuleta maandamano yasiyokoma. Nahusianisha uwiano huu usio sawa wa maendeleo na nadharia tajwa na gesi ya Mtwara. Serikali imeamua kufuata njia ya Center-Periphery kwa kuwanyima wananchi wa Mtwara fursa za ajira zitokanazo na mitambo ya kuchakata gesi na kufua umeme. Nisingependa kuingia kwenye mjadala wa kiasiasa zaidi kwenye hili, kwa sababu tayari wanasiasa wameshalijadili kwa undani. Je wananchi wa Mtwara walishirikishwa kwenye kuamua kujenga mifuo ya umeme Dar. Tujadili

No comments: