4/30/07

SAFISHA HAPA.....CHAFUA PALE!

UTANGULIZI

Ni suala la kawaida kukuta barafu/theluji katika miinuko ya maeneo mbali mbali ya nchi zilizo katika Tropiki ya Kansa, yaani nyuzi 23.26' kaskazini mwa Ikweta, hasa wakati wa majira ya baridi. Barafu/theluji huongezeka zaidi kama unazidi kuelekea kaskazini katika mzingo wa Aktiki (nyuzi 66.33'). Kwa wenyeji wa maeneo haya, huu ni msimu wa michezo ya wakati wa baridi kama vile kuteleza katika theluji na kutembea katika maji yaliyoganda (barafu). Lakini kwa watumiaji wa vyombo vya usafiri kama baiskeli, magari, treni na ndege ni msimu usiopendeza sana. Kwa upande wa baiskeli, magari na ndege, ni msimu wa kubadilisha magurudumu. Magurudumu yanayotumika wakati wa kiangazi ni tofauti na yale yatumikayo wakati wa baridi. Tofauti yake ni kwamba magurudumu ya msimu wa baridi huwa na misumari midogo midogo katika uso wake, ili kuleta msuguano wa kutosha (friction) wakati chombo kinapopita katika barafu ama theluji. Bila magurudumu ya namna hii ni rahisi sana kwenda nje ya barabara kama kuna theluji, kwa sababu huwa inateleza sana. Theluji pia hujaa katika reli na kusababisha utelezi. Ni kawaida kwa maeneo haya kukuta vyombo vya kusafisha theluji barabarani kila asubuhi.

UONDOAJI WA THELUJI
Theluji ikishafagiliwa, hukusanywa mahali na kisha kuzolewa katika magari makubwa na kwenda kutupwa. Shida yake huanzia hapa, kwamba mara nyingi katika nchi hizi theluji hutupwa katika bahari ama maeneo mengine ambayo ni oevu. Iwapo kunakuwa na joto theluji hii huyeyuka na kuwa maji. Wanamazingira hawapendezwi na suala hili la kutupa theluji na barafu katika maeneo haya. Madai yao ni kuwa, mara nyingi theluji inayokusanywa mitaani huwa na takataka sana, kwa hiyo unapoikusanya na kwenda kuimwaga baharini ama maeneo mengine unakuwa unasababisha uchafu mahali hapo. Ieleweke pia kuwa theluji hii huweza kuambatana na mafuta yanayotumika kulainishia ama kuendeshea mitambo, hivyo kama itatupwa katika maeno yenye unyevu basi itasababisha kufa kwa viumbe hai ambao hutegemea maji hayo kwa maisha yao kama vile samaki na vyura. Hali kadhalika mafuta huganda katika mbawa za ndege wavuvi, hivyo hushidwa kuruka kujitafutia riziki zao na hivyo hufa kwa njaa.

SULUHISHO
Kutokana na malalamiko ya wanamazingira kuhusiana na uchafuzi huu, wazoaji wa theluji (hasa halmashauri za miji) wameamua kutupa theluji hii katika maeneo maalum yalitengwa kwa ajili hiyo (dump sites). Kwa hiyo maeneo hayo huwa ni maalum kwa ajili ya kumwaga theluji na barafu na uchafu unaoambatana navyo. Bado wanamazingira hawajaridhika na kitendo hiki, kwa sababu wanasema unatibu tatizo moja huku ukisababisha jingine la uchafuzi wa mazingira. imsingi barafu na theluji ni maji, na wanaomwaga wanajua kuwa wakati wa kiangazi huwa inayeyuka, suala linalogombaniwa hapa ni taka zinazoambatana na theluji ama barafu, kuwa ndizo zinazoleta madhara katika mazingira. Mpaka sasa bado kuna mgongano wa mawazo kuhusu nini kifanyike ili kutatua mvutano huu, tusubiri tuone matokeo yake.
Kwa upande wa nchi za Kitropiki hakuna tatizo la barafu, katika miji, ila suala la utupaji ovyo wa taka lipo na limeshamiri sana.

Barafu iliyokusanywa, ikisubiri kuzolewa na kwenda kutupwa!

No comments: