10/23/06

NISHATI NA MAISHA

UTANGULIZI
Kwa dhana, nishati ni ule uwezo wa kufanya kazi au kitu fulani. Kuna nishati za aina mbalimbali kama vile joto, sauti, mwendo, mwanga na kadhalika. Kuna uwezekano mkubwa sana wa kubadilinishati hizi kutoka aina moja kwenda nyingine kwa kutumia mbinu na vifaa mbali mbali. Kwa mada hii nitaongelea kwa ufupi sana nishati za mwanga na joto.

UMUHIMU WA NISHATI
Kwa maelezo rahisi ni kwamba hakuna maisha bila nishati. Nishati ni chanzo cha uhai wetu, kwani nishati ya mwanga kama ule wa jua hutusaidia kuona na kufanya mambo mbali mbali, hutuletea vitamini D na pia nishati hii husaidia usanisi wa chakula cha mimea, ambayo nasi tunaitegemea kwa chakula chetu. Nishati ya mwendo hutusaidia kujongea kutoka mahali fulani hadi pengine kwa muda mfupi sana kwa teknolojia ya leo na nishati ya joto hutusaidia kwa mambo mbali mbali kama vile kuivisha chakula chetu, kukausha mazao, kurekebisha hali ya hewa majumbani na kadhalika.
Kumekuwa na mwamko mahali mbalimbali hapa ulimwenguni kuhusu mustakabali wa dunia hasa katika suala nyeti la nishati. Mara nyingi dunia imekuwa ikitegemea mimea, madini (makaa ya mawe na nyuklia) na mafuta kama vyanzo vikuu vya nishati za namna mbalimbali.

KUNI NA MKAA
Katika mimea tunapata kuni na mkaa ambavyo kwa nchi kama Tanzania huchangia zaidi ya asilimia tisini ya mahitaji yote ya nishati kwa taifa. Hiki ni kiwango kikubwa sana, kwa hiyo juhudi za makusudi zinatakiwa ili kupunguza kiasi hiki. Kuni hutumika na mkaa kila mahali katika nchi zinazoendelea katika kufanyia kazi mbali mbali, kuanzia majumbani hadi viwandani. Kuni hutumika kuzalisha nishati ya joto katika viwanda vya chai na tumbaku, hutmika kupikia majumbani na matumizi mengine mengi tu. Kwa nchi zilizoendelea kuni hutumika kuchemshia maji, ambayo husambazwa majumbani kwa mabomba maalum kwa ajili ya kuzalisha joto wakati wa baridi. Ni nishati tegemeo sana kwa nchi hizi hasa wakati wa baridi, kwa kuwa kutumia mitambo ya umeme kuzalisha joto ni ghali kwa kiasi fulani.

MAKAA YA MAWE
Makaa ya mawe kwa miaka ya nyuma yalitumika moja kwa moja viwandani kuzalisha nishati za joto na mwendo kwa matumizi mbali mbali. Mpaka sasa kuna maeneo kadhaa hapa duniani ambapo makaa ya mawe hutumika kuzalisha nishati (kama vile mgodi wa makaa ya mawe kule Ilima/KiwiraMbeya). Makaa pia hutumika katika viwanda vya saruji katika kuzalisha joto la kuyeyushia mawe ili yasagwe na kuzalisha saruji. Lakini kutokana na uchafuzi wa hali ya hewa, ikaonekana kuwa makaa si nishati rafiki wa mazingira yetu, hivyo kukafanyika mabadiliko makubwa sana ya kuiacha nishati hii kwa maeneo mengi. Lakini bado kuna nchi nyingi tu ambazo hazijaiacha nishati hii, ikiwemo nchi ya China ambayo inakuja juu katika maendeleo ya viwanda duniani. Mwelekeo na mkazo vikawa katika mafuta ya jamii ya petroli ambayo kwa sasa yanachukua nafasi kubwa sana katika maisha ya mwanadamu.

MAFUTA YA PETROLI
Mafuta haya yanatumika kuendesha mitambo ya namna mbali mbali pamoja na ile izalishayo umeme, maarufu kama jenereta. Magari, ndege, meli, baadhi ya treni, huendeshwa kwa nishati hii pia. Kadri muda unavyosonga, nishati hii nayo imeonekana si rafiki wa mazingira kama inatumika katika mazingira ambayo si muafaka. Moshi unaotokana na mafuta haya yanapotumika katika mitambo huwa na athari sana katika mazingira, kwa kuwa huongeza kiasi kikubwa sana cha hewa ya kaboni dayoksaidi katika anga na kuharibu utando wa ozoni. Matokeo yake ni kuwa kunakuwa na ongezeko la joto katika uso wa dunia, na ongezeko hili limeleta athari nyingi sana katika sehemu mbali mbali hapa duniani (nilishaliongelea hili katika mada zilizopita). hio ni moja, lakini pili ni kuwa iwapo kunatokea ajali majini na chombo kinachosafirisha mafuta kikahusika, mafuta hutapakaa katika maji (na kawaida mafuta huelea majini) na kuathiri viumbe wanaoishi katika maji. Kwa viumbe kama samaki, hushidwa kupumua kwa kuwa mafuta huzuia hewa kutoka na kuingia katika maji. Kwa ndege wanaoshi kwa kutegemea uvuvi, mara wapakaapo mafuta haya katika shughuli zao za uvuvi hushidwa kuruka kwa kuwa mbawa zao hushikamana na kukakamaa hivyo kwa wakati fulani hufa. Kwa sasa kuna mikakati kwa nchi zilizoendelea, kuachana na utegemezi wa nishati hii, lakini itachukua muda sana, ingawa inawezekena (rejea makala iliyopita).

MAJI
Kwa miaka mingi nguvu ya maji imekuwa ikitumika kwa namna mbali mbali. Kwa upande wa nishati, maji yamekuwa yakitumika moja kwa moja kuendesha mitambo ya kusagia nafaka, na kwa upande wa Tanzania bado mifumo hii inafanya kazi mpaka sasa. Kwa mfano, katika kijiji cha Kisiwani wilayani Muheza Mkoani Tanga, kuna mtambo wa kusagia nafaka ambao kuendeshwa kwa nguvu ya maji. Kwa upande wa pili, kutokana na maendeleo ya kiteknolojia, maji yanatumuka kuendeshea mitambo ya kuzalisha umeme, na kwa sasa dunia imekuwa tegemezi kwa nishati hii kwa kiasi kikubwa. Hli si shwari sana kwa upande wetu Tanzania, kutokana na maji kutokuwa ya kuaminika na kutokuwa na mfumo mzuri wa urejeshaji maji katika mabwawa mara baada ya kuyatumia. Pia hali ya hewa hasa suala la ukame limekuwa kikwazo kikubwa kwa uendelezaji wa nishati hii. Miradi mikubwa ya umeme wa nguvu ya maji si rafiki wa mazingira, kwa kuwa hutumia maeneo makubwa sana kuhifadhi maji, kwa hio kunakuwa na uhamishaji wa watu na wanyama na mara kadhaa husababisha mafuriko kwa watu waishio kando yake iwapo milango ya bwawa itafunguliwa kupisha matengenezo, kwa kuwa maji hufunguliwa kwa wingi sana. Pia miradi hii hutumia maji mengi sana, kwa hio viumbe wengine ambao hutegemea maji hayo mbele ya mabwawa hawapati maji kwa uhakika (kumbuka suala la vyura katika mradi wa umeme-Kihansi).

NYUKLIA
Ni moja ya nishati mbadala katika kupunguza tatizo la nishati. Kwa sasa ni nchi zilizoendelea tu ndizo zina uwezo na mamlaka ya kutumia nishati hii, kwa kuwa ni ghali sana. Pia inadhibitiwa sana na shirika na nguvu za nishati la Umoja wa Mataifa liitwalo 'International Atomic Energy Agency' (IAEA), kwa kuwa ni nishati hii hii itumikayo kutengeneza silaha za maangamizi, kwa hio wanahofia kuwa iwapo inaachwa bila ya udhibiti basi inaweza kutumika kwa malengo mengine, na si uzalishaji wa nishati. Kwa sasa nchi kama Japan, Korea Kaskazini, India, Iran*, Marekani, Norway na Urusi zinatumia nyuklia kwa kuzalishia nishati. Nyuklia huhitaji uangalizi wa hali ya juu sana, kwa kuwa ikivuja ina madhara sana kwa mwanadamu na viumbe wengine. Ajali ya kuvuja kwa mitambo ya nyuklia ilishawahi kutokea katika mji wa Chernobyl nchini Urusi mnamo mwaka 1986 na kusababisha madhara makubwa!
*(Vinu havijaanza kufanya kazi Iran)

UMEME WA MIONZI YA JUA
Ni teknolojia mpya kwa kiasi fulani, na ni rafiki wa mazingira. Ni mfumo wa kuvuna mionzi ya jua na kuzalisha umeme kwa kutumia mitambo maalum ijulikanayo kama 'Photovoltaics'. Uzalishaji wa umeme huu hutegemea sana uwepo wa mwanga wa jua na vihifadhi vya umeme huo kama betri. Umeme huu unafaa sana kwa mazingira yaliyo mbali na umeme wa gridi. Ni teknolojia ghali kwa kiasi fulani ingawa ni nzuri.

Kwa namna moja au nyingine tuendelee kujaribu kutafakari na kutafuta suluhisho la matatizo ya nishati yanayoikabili dunia, ili iwe mahali salama pa kuishi wanadamu.
Nafasi yako ni ipi katika hili?
Jadili!

10/11/06

MAFUTA MBADALA

UTANGULIZI
Kumekuwa na kilio sehemu mbali mbali duniani kuhusu uchafuzi wa hewa pamoja na athari zake ambazo dunia imeanza kuonja makali yake. Kilio hiki kinatokana na kuongezeka kwa kiwango cha moshi wenye sumu katika anga, na kuharibu mfumo mzima wa hali ya hewa. Athari zaidi zinaonekana katika utando wa 'ozone', ambao umetobolewa na hewa hizi za sumu. Kazi ya utando huu ni kuzuia mionzi ya jua yenye athari kutufikia moja kwa moja na kutuathiri. Athari ambazo dunia inazipata kwa sasa ni pamoja na ongezeko la joto duniani na kupungua kwa kiwango cha barafu katika milima, kupotea kwa baadhi ya jamii za mimea na wanyama kutokana na ongezeko hili la joto, ongezeko la magonjwa kama kansa na magonjwa mengine ya ngozi. Pia kuna maeneo ambapo utando wa moshi wa viwanda na magari ni mkubwa na hivyo husababisha mvua za tindikali. Mvua hizi hutokana na kuongezeka kwa hewa ya salpha dayoksaidi katika anga. Hewa hii ikizidi angani na kuchanganyikana na maji au unyevu hutengeneza tindikali ya salfarasi 'sulphorous acid', na hii ina madhara sana kwa mimea na wanyama. Tindikali hii huunguza majani ya mimea na kwa wanyama husababisha magonjwa ya ngozi. Kwa nchi za Ulaya ya Magharibi wanafahamu sana madhara ya mvua hizi za tindikali, kwani zimeharibu sana uoto wa asili. Kutokana na sababu hizi basi, kumekuwa na hatua mbali mbali za kupunguza hewa chafu katika anga, na moja ya hatua hizo ni kutumia mafuta mbadala ya kuendeshea mitambo badala ya mafuta ya jamii ya petroli.

MAFUTA MBADALA NI YAPI?
Msisitizo wa kutumia mafuta yasiyo na madhara sana kwa mazingira umekuwa ukipata kasi kadri siku zinavyosonga. Nchi zilizoendelea zimekuwa msitari wa mbele katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na uzalishaji mkubwa wa mafuta haya mbadala. Mafuta haya yanatokana na mimea kama mbono, miwa, michikichi, alizeti, maharage ya soya na mahindi. Kimsingi kila mmea una uwezo wa kutoa mafuta haya, kulingana na hali ya kiteknolojia iliyopo mahali husika. Mimea tajwa hapo juu, ukiacha miwa na mahindi, hutoa dizeli ambayo nchi zilizoendelea zinatumia kuendeshea mitambo ya namna mbalimbali. Miwa hutoa kimiminika kiitwacho 'ethanol' na hii kutumika sana kuendeshea mitambo pia. 'Ethanol' ni jamii ya pombe inayotengenezwa kwa njia ya mvukizo au mvuke. Kwa jina lingine rahisi hii ni 'gongo' ya kiwandani. Ni nyepesi sana na inashika moto haraka, hivyo wataalamu wameona inafaa kwa mitambo. Kumbuka kuwa karabai zinawashwa kwa mafuta ya jamii hii.

WAZALISHAJI WA MAFUTA MBADALA
Kwa upande wa 'ethanol', wazalishaji wakubwa kwa soko la dunia ni Brazili na Marekani na walianza karibu miaka ishirini iliyopita. Hawa wanazalisha bidhaa hii kutokana na makapi ya viwanda vya miwa. Pia nchi za umoja wa Ulaya ni wazalishaji wakubwa wa bidhaa hii. Kwa upande wa dizeli ya mimea, wazalishaji vinara ni Malaysia, China na Ujerumani. Malaysia ni mzalishaji wa kwanza wa mafuta ya mawese duniani, na dizeli wanayotengeneza inatokana na mawese. Wachina wanatengeneza 'ethanol' kutokana na mihogo na wanapata shehena kubwa ya mihogo hii kutoka Vietnam, Thailand na Indonesia.
Kwa upande wa Brazili, kuna magari milioni tatu yanayotumia ethanol! Wakati huo huo kuna magari milioni moja na laki tatu yanayotumia mchanganyiko wa petroli na ethanol.
(Chanzo cha takwimu: UNIDO/Berkeley BC Aprili 2006)

FAIDA ZA MAFUTA MBADALA
Mafuta haya hayatoi moshi wenye athari kwa anga, kwa kuwa hayana viambata vyenye sumu, kulinganisha na mafuta ya jamii ya petroli. Mafuta ya petroli huchanganywa na madini ya risasi 'lead' na hivyo yakitumika katika mitambo hutoa moshi wenye sumu katika anga.
Kwa kuwa mafuta mbadala hutokana na mimea, huongeza kipato kwa wakulima wa mazao yatoayo mafuta haya. Utengenezaji wa dizeli mbadala hauhitaji teknolojia za hali ya juu sana, tofauti na mafuta ya jamii ya petroli, hivyo hata nchi zinazoendelea zinaweza kumiliki mitambo ya kuzalishia mafuta haya.

TANZANIA NA MAFUTA MBADALA
Kumekuwa na tafiti mbalimbali zinazofanywa na watu na taasisi anuwai nchini Tanzania, kuhakikisha kuwa kunakuwa na maendeleo katika uzalishaji wa dizeli ya mimea. Baadhi ya taasisi zilizofanya utafiti wa mafuta haya ni pamoja na shirika la Msaada wa Kiufundi la Ujerumani (GTZ), Kampuni ya Kukuza Teknolojia (KAKUTE) ya Arusha na Taasisi ya Kuendeleza Nishati Endelevu na Mazingira Tanzania (TaTEDO). Kwa upande wa KAKUTE, wao wanafanya uzalishaji mdogo wa dizeli inayotokana na mbono, pamoja na kutengeneza sabuni zake.
Iwapo kutakuwa na msisitizo kwa watu binafsi, mashirika na serikali katika kuzalisha mafuta haya, basi tutaondokana na umasikini, kwa sababu bidhaa hii kwa sasa ina malipo mazuri katika soko la dunia. Nasema hivi kwa sababu tayarai nchini Tanzania tuna viwanda kadhaa vya miwa ambavyo hutoa makapi mengi ya kuweza kuzalisha ethanol na wakati huo huo mimea ya mbono husitawi hata katika maeneo yenye ukame.
Ni kitu kinachowezekana, ila inataka utashi!
Nafasi yako katika hili unaitumia kikamilifu?
Jadili!