12/14/06

SUALA HILI LINATUFUNDISHA NINI?



Katika pitapita yangu katika nchi hizi za Ulaya ya Magharibi mara nyingi nimekuwa nikikutana na changamoto za namna mbalimbali pamoja na vioja kadhaa. Lakini suala kubwa sana ambalo limenishtua sana na kunikera kiasi fulani ni kukuta wanyama wa aina mbali mbali katika hifadhi maalum “zoo” jijini Copenhagen nchini Denmark ambao aghalabu hupatikana katika uwanda wa kitropiki pamoja na Ikweta. Matarajio yangu mimi yalikuwa ni kwenda pale katika hifadhi kuangalia wanyama ambao wanapatikana katika nchi za baridi kama dubu, “moose, seals, llama, walrus” na kadhalika ambao sikupata kuwaona wakati natembelea mbuga zetu kwa kuwa hawapatikani kwetu katika nchi za joto. Wanyama hawa ambao niliwakuta katika hifadhi ya jiji tajwa hapo juu ni kama vile swala wa aina mbali mbali, vifaru, twiga, nyumbu, kangaroo, simba, nyani, ngedere, sokwe na ndege wa aina mbalimbali kama vile korongo, heroe batamaji na kadhalika. Wanyama hao pichani, pamoja na wengine ambao sijachapisha picha zao hapo niliwakuta katika hifadhi tajwa. Sasa sijajua kama wanyama hawa wapo hapa kihalali ama wamebebwa kwa njia ambazo wao wenyewe wanazijua Kwa hiyo basi kwa miaka michache sana ijayo halitakuwa suala la ajabu sana kukuta sisi ambao tunatoka katika uwanda wa kitropiki tunakwendaUlaya na kutazama wanyama ambao kwa asili walikuwa kwetu, ila kutokana na sababu ambazo mimi binafsi sijazifahamu wamehamia katika nchi za baridi. Kusema kweli hiki ni kioja ingawa najua kuna baadhi ya watu hawaoni athari za suala hili kwa uchumi kama wa nchi zetu changa ambazo bado tunahitaji pesa za watalii kwa kiasi kikubwa. Naomba utazame picha hizo (ambazo nilizipiga Ulaya, sio Serengeti) na utoe mtazamo wako, kwamba iwapo simba, twiga, nyumbu, nyati na wanyama wengine wa Afrika na Asia wanapatika nchi za baridi za Ulaya, kuna haja gani ya watalii kwenda Afrika, Amerika ya Kusini na Asia kutazama wanyama hawa wakati wanapatikana kwao?
Jadili!

11/27/06

EBPA- MFANO WA KUIGWA!

UTANGULIZI
EBPA ni ufupisho wa ’Environment- Based Poverty Alleviation’. Hii ni taasisi isiyo ya kiserikali ambayo kazi yake kuu ni ulinzi wa mazingira, lakini kwa namna ya pekee, kama ambavyo nitafafanua hapa chini. Taasisi hii ina makao yake makuu jijini Dar Es Salaam na inaongozwa na Bwana Charles Lugenga.

MALENGO YA TAASISI
Kwa mujibu wa Bwana Lugenga lengo kuu la taasisi hii ni kutunza mazingira kwa namna ya pekee, kwa kukusanya sehemu ya taka zilizotupwa na kutengeneza vitu vingine kwa matumizi mbali mbali. Taka ambazo hukusanywa kwa wingi ni kama makopo ya vinywaji baridi, makopo ya vinywaji vikali, chupa za maji pamoja na vizibo vyake, vitunza-takwimu (diskettes), kadi za simu zilizotumika, magurudumu machakavu ya magari, mifuko mikubwa ya nailoni (viroba) pamoja na nembo za bidhaa mbali mbali (labels) na kadhalika. Katika maelezo yake, Bwana Lugenga anasema kuwa pamoja na kwamba si rahisi kukusanya kila taka lakini angalau kwa kiasi fulani tunaweza kupunguza uchafuzi wa mazingira kwa kutumia tena, kupunguza ingi wa taka na kurejesha. Anasema kuwa katika taasisi yake wanatumia mfumo wa ‘R3’ yaani ‘Reduce, Reuse, Recycle’ kwa maana ya kupunguza ukubwa au uwingi wa taka, kutumia tena taka kwa matumizi tofauti na ya mwanzo na kurejesha. Anasema kwa mfumo huu, kiwango cha taka kinachotupwa katika mazingira yetu kinakuwa na athari kidogo sana, tofauti na iwapo kama taka hizo zingetupwa bila kupitia hatua hizo. Anafafanua kuwa, kwa mfano ukichukua makopo ya vinywaji ukayakata na kutengeneza mikoba ama vikapu hutumii sehemu zote za kopo ila sehemu ndogo tu. Sasa basi hapa umekuwa umepunguza ukubwa wa taka, kwa hiyo unakuwa umepunguza pia athari.

BIDHAA ZITOKANAZO NA TAKA
Kuna bidhaa mbali mbali ambazo EBPA wanatengeneza kutokana na taka. Bidhaa hizo ni mavazi kama makoti, mataji na kofia zilizotengenezwa kwa makopo ya vinywaji, nembo ama vitunza takwimu vilivyotumika na kadi za simu zilizotumika. Katika hali ya kushangaza Bwana Lugenga na taasisi yake wamejenga nyumba kwa magurudumu yaliyotumika katika jiji la Dar es Salaam katika eneo la Pugu. Kuhusu suala la nyumba hii ya magurudumu, anasema kuwa anafanya mawasiliano na watu wa Kitabu cha Kumbukumbu cha Guinness ili apate kuweka kumbukumbu ya nyumba hii kuwa ya kwanza ya aina yake kutengenezwa kwa magurudumu kuanzia chini mpaka katika paa. Pia ni kawaida kumkuta bwana Lugenga akiwa na ama mkoba au kikapu kilichotengenezwa kwa bidhaa tajwa hapo juu popote pale alipo, kwa hiyo hatengenezi bidhaa zake kwa maonyesho, ila kwa matumizi. Anasema kuwa, chupa za plastiki za maji ya kunywa huokotwa na kupelekwa katika kiwanda cha TIRDO kilichopo Msasani. Chupa hizi husagwa na kutumuka kutengenza bidhaa mbali mbali, na kuna wakati malighafi itokanayo na chupa hizi hupelekwa nje ya nchi ambako kuna soko zuri. Pia bidhaa kama madumu yaliyotumika hukusanywa na kupelekwa mahali hapo, husagwa na kurejeshwa viwAndani ambapo hutumika kwa kazi mbali mbali.


UREJESHAJI WA TAKA
Uwapo njiani kama unatokea Ubungo kwenda Mwenge kabla hujafika njiapanda ya kwenda Survey mkono wa kushoto, utakuta kundi la vijana wakiwa wamekusanya chupa za maji na bidhaa nyingine za plastiki. Licha ya mahali hapa, kuna maeneo mengine mengi tu ambapo vijana wamejiari katika ukusanyaji wa taka za namna hii. Bidhaa hizi hupelekwa katika Kiwanda cha kurejesha taka ambacho nimekitaja hapo juu. Nilitembelea kiwanda hiki mnamo mwezi Mei 2006 na kukuta bidhaa mbali mbali zikiwa katika hatua mbali mbali kuelekea katika urejeshwaji. Licha ya taka, bidhaa ambazo hazikutengezwa vizuri kutoka katika viwanda mbali mbali vinavyojihusisha na utengenezaji wa bidhaa za plastiki hupelekwa mahali pale ili kurejeshwa na kutengeneza bidhaa nyingine.
Inawezekana pia kuwa kuna taasisi mbali mbali zinazofanya kazi kama taasisi hii ya EBPA mahali mbali mbali nchini mwetu, ni vizuri iwapo tutawaunga mkono kwa namna anuwai ili kuweza kujikwamua kiuchumi na kulinda mazingira.

Inawezekana, tutimize wajibu wetu

11/24/06

USHAURI KUNTU KWA WAMILIKI WA MABASI!

UTANGULIZI
U hali gani msomaji wa safu hii. Katika makala zilizopita, niliwahi kugusia kidogo suala la uchafuzi wa mazingira hasa kwa mabasi makubwa ya masafa marefu, kuhusu utupaji wa taka kwa abiria wanaokuwa wakiabiri katika mabasi hayo. Leo nitafafanua kwa undani kidogo jinsi ya kufanya, ili kuweza kukabiliana na uchafuzi wa mazingira hasa kwa wenye mabasi. Ni ushauri tu, wana haki ya kuuchukua ama kuuacha, ni hiari yao lakini ni muhimu sana kama watauzingatia.

MADA
Katika makala niliyodondoa hapo juu katika utangulizi, nilisema kwamba ni kawaida kwa mtu yeyote anayesafiri kwa mabasi makubwa ya masafa marefu kukuta mifuko ya plastiki ikiwa imezagaa njiani, kando ya barabara hizi kubwa. Aghalabu mifuko hiyo hupatikana maeneo ambayo huwa hayana watu. Sasa huwa tunajiuliza nani huwa anatupa mifuko hiyo? Jibu ni 'Wasafiri' ama abiria. Ni jambo la kawaida sana kukuta katika kila basi kubwa la masafa marefu lina hifadhi ya mifuko ya plastiki ndani. Aghalabu mifuko hii hutumika kuwakinga baadhi ya abiria ambao hutapika njiani, labda kutokana na ugonjwa ama misukusuko ya gari wawapo njiani. Sasa basi, mara abiria wanapokuwa wamemaliza kutapika, hutupa mifuko hii nje ya basi kupitia madirishani. Vitendi hivi huchangia sana kuchafua mazingira, kwani mifiko hii ya plastiki ina athari sana kwa mazingira.
Hali kadhalika, nilijadili kuwa dakika kumi ambazo wenye mabasi hutoa kwa abiria kwa ajili ya kula na kujisaidia huwa hazitoshi. Hii ni kwa sababu, abiria hutumia muda kama dakika tatu mpaka tano kutoka nje ya basi waendapo kula. Sasa basi abiria wa mwisho kutoka katika basi husika kwa maana hii atatumia dakika tano zilizobaki kujisaidia, kupanga msitari katika kuagiza chakula, kula na kama inawezekana kwenda katika duka kununua maji ya kunywa. Katika hali ya kawaida, utaona kuwa muda huu hautoshi hata kidogo. Kwa hiyo basi abiria walio wengi hulazimika kubeba chakula katika mifuko na kwenda kula ndani ya gari. Matokeo yake, masalia ya vyakula pamoja na mifuko hutupwa nje ya basi na kuhatarisha mazingira. Hali kadhalika, iwapo mtu mwenye ugonjwa wa kuambukiza kama kipindundupindu ama homa za matumbo atatapika katika gari na kutupa matapishi nje ya basi, kunakuwa na uwezekano mkubwa wa kusambaza ugonjwa huo katika maeneo ambapo matapishi hayo yanakuwa yametupwa. Hii ni hatari sana, ingawa sote tunaonekana kama tunafumbia macho tatizo hili. Nilitoa wito kuwa tuwaige watunza hifadhi wa mbuga ya wanyama ya Mikumi, mkoani Morogoro, huwa wanajitahidi sana kutoa elimu kwa abiria pamoja na kusafisha uchafu wote utupwao mbugani hapo. Kuna matangazo mengi sana mbugani hapo, yakisisitiza kutotupa taka ovyo katika mbuga hiyo.

USHAURI
Kwanza,ni vyema kama katika kila basi kukawa na sehemu ya kutunzia taka, kwa maana ya kwamba taka zote katika basi husika zikusanywe na kuhifadhiwa katika buti ya basi. Mara wafikapo kituoni, watumishi wa basi husika inabidi watupe taka hizi katika ghuba za kutupia taka ama mahali pengine palipoandaliwa maalumu kwa ajili ya kuhifadhi taka. Si ustaarabu hata kidogo kutupa taka ovyo njiani. Pili, inabidi ila basi liweke matangazo kuwajulisha abiria kuwa ni marufuku kutupa taka nje ya basi. Matangazo haya yaende sambamba na msisitizo wa kuwa na sehemu ya kuhifadhi taka katika basi, kwani kama hakuna sehemu ya kuhifadhi taka katika basi, unakuwa vigumu kwa abiria kutekeleza amri hizo. Tatu, kuwe na matangazo katika vituo vya mabasi haya kila mkoa, yanayohusu usafi kwa abiria wanapokuwa wakisafiri na mabasi hayo. Katika makala hii nimesisitiza sana suala la mabasi makubwa kwa sababu ndio yenye kuchafua sana njia zetu pamoja na mzingira kwa ujumla. Nne, serikali itunge sheria kali za kuwabana wamiliki ma watumishi wa mabasi kutotupa taka ovyo njiani na kwamba wawe na sehemu maalumu ya kuhifadhi taka katika mabasi.

Mbona wenye ndege wameweza, kwa nini hawa wamiliki wa mabasi wanashindwa?
Jadili

MALENGO YA MAENDELEO YA MILENIA - 2: LENGO NAMBA SABA

UTANGULIZI
Katika makala zilizopita niliongelea malengo ya milenia ambayo kwa ujumla wake yapo nane, pia niliahidi kujadili lengo namba saba kwa undani na wasaa huo ni sasa. Lengo hili kwa Kiingereza limeandikwa ‘Ensure Environmental Sustainability’. Kwa tafsiri yangu katika Kiswahili nasema ‘Kuzingatia Uendelevu wa mazingira’. Katika ufafanuzi wake, walioandika lengo hilo wanasema lazima tuingize suala la mazingira katika mfumo wetu wa maendeleo endelevu katika sera na mipango ya nchi zetu na kurejesha rasilmali katika mfumo wake wa asili. Hii ina maana ya kwamba katika suala zima la maendeleo, huwezi kukwepa suala la mazingira, ndio sababu likapewa umuhimu wa pekee katika muktadha wa malengo ya milenia. Kwa ujumla wake, mazingira ni vitu vyote vinavyomzunguka mwanadamu. Ni mara nyingi sana katika shughuli zetu za uzalishaji mali tumekuwa tukichukua rasilmali nyingi katika mazingira yetu bila kurejesha kwa kiasi Fulani kama ninavyofafanua hapa chini.

1. ARDHI
Ardhi ndio mama wa kila kitu kiasi kwamba wataalamu tukaamua kuiita ‘Mother nature’. Bila ardhi hakuna maisha. Tumekuwa tukichukua rasilmali nyingi sana katika ardhi, mara nyingine bila kuzingatia uendelevu wake. Tunachukua mimea, wanyama, maji na madini bila kuchukua tahadhari za kimazingira na kujali madhara yajayo baada ya hapo. Madini yaliyo mengi yanapatikana ardhini na namna pekee ya kuyapata ni kuyachimba toka humo ardhini yalimo. Lakini kwa utovu wetu wa nidhamu tunaacha kufukia mashimo na kurejesha sehemu ya mimea na wanyama walioondolewa mahali hapo kwa makusudi. Tunamkomoa nani? Kwa mtazamo wangu sidhani na sipendi kuamini kuwa tunakuwa hatufahamu tunachokifanya. Matokeo ya madhara haya tunayapata hapa hapa, kwani kumekuwa na upungufu wa maji maeneo mbali mbali duniani, kwani katika shughuli zetu tunaharibu mzunguko wa maji. Pia kumekuwa na upotevu wa viumbe hai sehemu nyingi tu. Kwa kawaida ardhi, mimea na maeneo yenye unyevu yapatapo joto na mwanga wa jua hupumua.Katika kupumua huku mvuke huo huenda angani na kuganda na kufanya mawingu ambayo baadaye hurudi ardhini kama mvua, theluji, barafu na mzunguko huendelea. Sasa basi iwapo sehemu fulani ya mzunguko huu itaathirika kwa namna moja au nyingine basi athari hizi zitasambaa hata katika sehemu nyinginezo za mzunguko huu. Hivi ndivyo mfumo mzima ulivyo. Suala la kilimo pia ni la kuangaliwa. Kumekuwa na matumizi makubwa sana ya mbolea za viwandani katika shughuli za kilimo, hasa katika nchi zinazoendelea. Mbolea hizi,kwa namna moja au nyingine zinachosha sana ardhi, kiasi kwamba baada ya muda fulani ardhu husika inakuwa haina uwezo tena wa kuzalisha mazao mengi kama mwanzo. Wao wenyewe wanaotengeza mbolea hizi wanazipiga vita kwa sasa, sasa sijajua wanamtengenezea nani. Wameshajua kuwa zina madhara, hivyo wanataka kutumia mbolea asilia tu mashambani kwao. Kwa hiyo basi na sisi inabidi tubadilike na kutumia mbolea zinazotengenezwa kiasili kama samadi na mboji ili kulinda ardhi yetu. Licha ya mbolea, suala la kulima milimani ni la kuangaliwa, kwani husababisha mmomonyoko wa ardhi iwapo mvua itanyesha katika maeneo haya. Kuna tovuti kadhaa zimeelezea kinagaubaga suala hili pamoja na lile la kuzidisha idadi ya mifugo katika eneo dogo na kuzidisha madhara katika eneo husika, vitendo ambavyo huchangia kwa kiasi kikubwa kuharibu ardhi na mazingira kwa ujumla. Kwa hiyo sitayaongelea kwa undani sana masuala haya. Inafaa tu kuyaachia majanga ya asili kama vile volkano na matetemeko ya ardhi yaharibu uasilia wa ardhi, na siyo sisi wanadamu kuiharibu kwa makusudi, kwani kwa kufanya hivyo tunajichimbia kaburi.

2. MAJI
Kumekuwa na kauli mbiu kuwa ‘Maji ni Uhai’. Hakuna ubishi katika hili, bila maji hakuna uhai. Lakini je rasilmali hii tunaitumiaje? Sidhani kama tunafanya juhudi za kutosha katika kuhakikisha kuwa tuna matumizi endelevu ya rasilmali hii. Kwanza, katika kilimo huwa tunatumia mbolea za viwandani. Mbolea hizi si zote huchukuliwa na mimea kwa ajili ya utengenezaji wa chakula. Sehemu ya mbolea hupotelea ardhini na kuchafua hifadhi ya maji katika miamba ijulikanayo kama ’aquifers’. Kitendo hiki kwa lugha ya kitaalamu hufahamika kama ’Leaching’. Hatuwezi kuona kwa macho kwa sababu kitendo hiki hufanyika chini ya ardhi, kwa hiyo huhitaji vipimo vya kitaalamu kujua madhara yake katika maji na maisha ya wanadamu kwa ujumla. Katika kilimo hicho hicho, dawa za kuulia magugu na wadudu waharibifu wa mazao mashambani pia huchangia madhara katika maji kwani dawa hizi mara nyingi huenda katika maji iwapo mvua itanyesha katika mashamba yaliyowekwa dawa hizi. Pili, maji ya bahari ndio yamekithiri kwa uchafu, na ndio humo humo tunapata samaki kwa ajili ya kitoweo. Maji machafu ya miji yote ambayo iko kando ya bahari huishia baharini, maji taka ya viwanda ambavyo hupakana na bahari hali kadhalika huishia baharini. Taka za sumu toka viwandani humwagwa baharini. Hali hii pia iko katika maziwa na mito, ingawa si kwa kiasi kikubwa sana kama baharini. Inasemekana kuwa kwa nchi zinazoendelea kama yetu, baadhi ya wavuvi hutumia mabomu katika shughuli zao za uvuvi. Kitendo hiki si tu kwamba kinaua mazalia ya samaki, bali pia ni chanzo kikubwa cha uchafuzi wa maji. Baruti itengenezayo mabomu ni kemikali yenye sumu, sasa basi iwapo itachangayikana na maji, basi sumu hizi huturudia sisi wenyewe aidha kwa kula samaki waliovuliwa kwa mabomu au kwa kunywa moja kwa moja maji hayo. Lakini kwa tamaa zetu za kupata pesa za haraka, tunasahau madhara ya muda mrefu kama haya na kuishia kushibisha matumbo yetu kwa uvuvi wa mabomu. Tatu, kuna ujenzi na kilimo katika vyanzo vya maji. Kama tunayofahamu, vyanzo vya maji ni muhimu kwa maisha yetu, kwa hiyo iwapo tunachafua hatumkomoi mtu, ila ni sisi wenyewe. Nimeliongelea kwa urefu sana suala hili katika makala zilizopita. Katika hali ya kawaida, inatakiwa tuyasafishe maji yaliyotumika majumbani na viwandani ili yaweze kutumika tena kwa shughuli nyingine, lakini tulio wengi hatuna utaratibu huu. Laiti kama tungezingatia suala hili basi uhaba wa maji kwa maeneo mbali mbali ingekuwa ni hadithi tu. Pia hatuna utaratibu wa uvunaji wa maji ya mvua, kwa maeneo mengi ya nchi zinazoendelea. Maji yanayopotea wakati wa mvua ni mengi sana, iwapo tungeyavuna na kuyahifadhi basi tungetatua suala la uhaba wa maji ambalo ni kubwa sana sehemu mbali mbali duniani. Nne, kama itakumbukwa, hivi karibuni wakati nchi ya Israeli ikiwa katika mgogoro na Lebanon, ilipasua kwa makusudi bomba la mafuta kando ya bahari na mafuta yote yaliyokuwa yanasafirishwa katika bomba hilo yakasambaa baharini na kuua viumbe wengi sana wanaotegemea maji hayo ya bahari. Hali hii ilileta usumbufu pia kwa vyombo vinavyosafiri majini katika maeneo hayo. Kitendo hiki ni cha kulaaniwa sana na kila mtu ambaye anajali usafi wa bahari na mazingira kwa ujumla, lakini cha ajabu hakuna hatua za kinidhamu zinazochukuliwa kukomesha tabia hii.


3. HEWA
Madhara ya uchafuzi wa hewa ni rahisi sana kusambaa kwa muda mfupi katika dunia hii. Hii inatokana na sababu kuwa hewa husafiri haraka sana hasa pale inapopata joto. Si ajabu basi iwapo hewa itachafuliwa katika bara fulani na madhara yakajiri katika bara lingine kwa muda mfupi sana. Tumesikia na kuona madhara ya uchafuzi wa hewa, hasa kuharibika kwa hewa ya ’ozone’. Niliongelea kwa kirefu suala hili katika makala zilizopita. Ikumbukwe kuwa kuna makubaliano yalifanyika katika mji wa Kyoto nchini Japan hasa kwa nchi tajiri, kuhusu kupunguza kiwango cha hewa zenye sumu toka viwandani kwenda angani. Hizi ni nchi za G8 zenye viwanda vingi na vikubwa ambavo huchafua sana hali ya hewa, hivyo ilikuwa ni hatua muhimu sana katika suala ziama la kutunza mazingira. Kama kawaida, Wamarekani hawakusaini mkataba huu wa makubaliano, kwa madai kwamba kusaini mkataba huo ni kukubali kuua uchumi wao ambao hutegemea sana viwanda hivyo. Wakaitwa tena nchini Afrika Kusini, wakakataa kwa mara nyingine tena kusaini mkataba huu. Kwa mara nyingine mwaka huu 2006, mwezi wa kumi na moja wamekataa tena kusaini mkataba huo na kurudisha nyuma kabisa juhudi za kupunguza uchafuzi wa hewa. Nchi nyingine zenye viwanda vingi kama Japan, Sweden, China, Ujerumani, Urusi na Denmark wameshaanza kupunguza kwa kiwango cha kuridhisha, uchafuzi wa hewa.

MIKAKATI ENDELEVU
Kuna mambo kadhaa ambayo yanapaswa kuzingatiwa iwapo tunataka kupata matokeo mazuri ya ya kile tunachokipanga.

SIASA DHIDI UTAALAMU!
Kwanza, tupunguze kama si kuacha kabisa kutatua matatizo ya kiufundi kwa mbinu za kisiasa. Pamoja na kwamba siasa inatawala maisha yetu ya kila siku, lakini si matatizo yote yanaweza kutatuliwa kisiasa. Suala la uchafuzi wa hali ya hewa ni la kiufundi, sasa iwapo tunataka kutatua suala hili kwa mbinu za kisiasa ni makosa makubwa sana kwani masilahi ya kisiasa ni ya muda tu. Matatizo kama njaa, ukosefu wa umeme, ukimwi, ukosefu wa maji, uharibifu wa rasilmali na ukosefu wa maadili ni matatizo ya kiufundi, hayapaswi kutatuliwa kisiasa. Yatatuliwe kiufundi kwani naamini kuna wataamu wengi tu wa utatuzi wa matatizo haya, wapewe nafasi. Umbumbumbu (au ni ubabe?) wa Marekani kukataa kusaini mkataba wa Kyoto wa kupunguza uchafuzi wa hali ya hewa inatakiwa ukemewe na kila mtu anayependa maendeleo ya muda mrefu na si maslahi ya kisiasa. Nasisitiza tena kuwa siamini wala sifikiri kuwa Wamarekani hawajui wanachokifanya katika hili suala la Kyoto. Nina imani kuwa huenda suala hili likapewa umuhimu wa kipekee na wale waliochukua madaraka nchini humo hivi karibuni, tuvute subira.

MAZINGIRA KWANZA, PESA BAADAYE!
Pili, ningependa kuongelea suala la mirahaba ya madini. Kumekuwa na maelezo mbali mbali kutoka kwa wadau wa madini kuwa tunalipwa mirahaba kutokana na madini yanayochimbwa nchini mwetu. Ni sawa kuwa tunapata mirahaba lakini vipi maslahi ya uhai wa hapo baadaye? Kama nilivyoongelea hapo juu, tusiangalie suala la pesa ambalo ni la muda mfupi ila tuangalie matokeo ya kuacha mahandaki katika machimbo ya madini. Nini kitatokea katika miongo kadhaa ijayo iwapo hali itaendelea kuwa kama hivi? Nani ataathirika? Wanaochimba madini sasa kwa teknolojia za kisasa zisizojali mazingira na uhai wetu watakuwa wameshaondoka na faida na kutuachia mashimo ambayo hayatakuwa na msaada wowote kwa wakati huo ambao vizazi vitakavyokuwepo (huenda hata sisi ) vitakuwa havina maji wala miti. Tuige mfano wa hatua zilizochukuliwa katika kuzuia uharibifu wa vyanzo vya maji na mazingira , kutokana na uchimbaji wa madini katika msitu wa Balangai wilayani Lushoto mkoani Tanga.
Sipendi kuonekana naingilia masilahi ya baadhi watu katika jamii kwa kupinga uchimbaji wa madini, lakini naongelea suala hili katika muktadha wa kitaalamu zaidi. Watakaopenda kuongelea suala hili katika muktadha wa kiuchumi wanaruhusiwa pia. Unafikiri ni kwa nini hao wanaotaka kuchimba madini katika nchi yetu hawaendi nchi zingine zenye madini kama sisi? Suala ni kwamba nchi hizi wana sera na sheria endelevu sna kuhusu mazingira.

UTASHI WA KISIASA
Kutatua matatizo yanayoikabili dunia kwa sasa kunahitaji utashi wa kisiasa na si utatuzi wa kisiasa. Katika kutekeleza malengo ya milenia, kinachotakiwa zaidi ni utashi huu ninaouongelea, kwani kwa utashi matatizo haya yanatatulika kabisa. Mpaka sasa inasemekana kuwa hazijaonekana juhudi za makusudi katika kutatua matatizo yaliyoanishwa katika malengo ya milenia, kiasi kwamba huo mwaka 2015 wa matazamio huenda mengi kati ya malengo hayo yasiwe yametimizwa. Wewe masomaji wa makala hii pamoja na mimi inapaswa tutimize wajibu wetu katika kuyafanikisha malengo haya, kwani inawezekana kabisa kuyafikia.
Soma hapa kwa habari zaidi.

10/23/06

NISHATI NA MAISHA

UTANGULIZI
Kwa dhana, nishati ni ule uwezo wa kufanya kazi au kitu fulani. Kuna nishati za aina mbalimbali kama vile joto, sauti, mwendo, mwanga na kadhalika. Kuna uwezekano mkubwa sana wa kubadilinishati hizi kutoka aina moja kwenda nyingine kwa kutumia mbinu na vifaa mbali mbali. Kwa mada hii nitaongelea kwa ufupi sana nishati za mwanga na joto.

UMUHIMU WA NISHATI
Kwa maelezo rahisi ni kwamba hakuna maisha bila nishati. Nishati ni chanzo cha uhai wetu, kwani nishati ya mwanga kama ule wa jua hutusaidia kuona na kufanya mambo mbali mbali, hutuletea vitamini D na pia nishati hii husaidia usanisi wa chakula cha mimea, ambayo nasi tunaitegemea kwa chakula chetu. Nishati ya mwendo hutusaidia kujongea kutoka mahali fulani hadi pengine kwa muda mfupi sana kwa teknolojia ya leo na nishati ya joto hutusaidia kwa mambo mbali mbali kama vile kuivisha chakula chetu, kukausha mazao, kurekebisha hali ya hewa majumbani na kadhalika.
Kumekuwa na mwamko mahali mbalimbali hapa ulimwenguni kuhusu mustakabali wa dunia hasa katika suala nyeti la nishati. Mara nyingi dunia imekuwa ikitegemea mimea, madini (makaa ya mawe na nyuklia) na mafuta kama vyanzo vikuu vya nishati za namna mbalimbali.

KUNI NA MKAA
Katika mimea tunapata kuni na mkaa ambavyo kwa nchi kama Tanzania huchangia zaidi ya asilimia tisini ya mahitaji yote ya nishati kwa taifa. Hiki ni kiwango kikubwa sana, kwa hiyo juhudi za makusudi zinatakiwa ili kupunguza kiasi hiki. Kuni hutumika na mkaa kila mahali katika nchi zinazoendelea katika kufanyia kazi mbali mbali, kuanzia majumbani hadi viwandani. Kuni hutumika kuzalisha nishati ya joto katika viwanda vya chai na tumbaku, hutmika kupikia majumbani na matumizi mengine mengi tu. Kwa nchi zilizoendelea kuni hutumika kuchemshia maji, ambayo husambazwa majumbani kwa mabomba maalum kwa ajili ya kuzalisha joto wakati wa baridi. Ni nishati tegemeo sana kwa nchi hizi hasa wakati wa baridi, kwa kuwa kutumia mitambo ya umeme kuzalisha joto ni ghali kwa kiasi fulani.

MAKAA YA MAWE
Makaa ya mawe kwa miaka ya nyuma yalitumika moja kwa moja viwandani kuzalisha nishati za joto na mwendo kwa matumizi mbali mbali. Mpaka sasa kuna maeneo kadhaa hapa duniani ambapo makaa ya mawe hutumika kuzalisha nishati (kama vile mgodi wa makaa ya mawe kule Ilima/KiwiraMbeya). Makaa pia hutumika katika viwanda vya saruji katika kuzalisha joto la kuyeyushia mawe ili yasagwe na kuzalisha saruji. Lakini kutokana na uchafuzi wa hali ya hewa, ikaonekana kuwa makaa si nishati rafiki wa mazingira yetu, hivyo kukafanyika mabadiliko makubwa sana ya kuiacha nishati hii kwa maeneo mengi. Lakini bado kuna nchi nyingi tu ambazo hazijaiacha nishati hii, ikiwemo nchi ya China ambayo inakuja juu katika maendeleo ya viwanda duniani. Mwelekeo na mkazo vikawa katika mafuta ya jamii ya petroli ambayo kwa sasa yanachukua nafasi kubwa sana katika maisha ya mwanadamu.

MAFUTA YA PETROLI
Mafuta haya yanatumika kuendesha mitambo ya namna mbali mbali pamoja na ile izalishayo umeme, maarufu kama jenereta. Magari, ndege, meli, baadhi ya treni, huendeshwa kwa nishati hii pia. Kadri muda unavyosonga, nishati hii nayo imeonekana si rafiki wa mazingira kama inatumika katika mazingira ambayo si muafaka. Moshi unaotokana na mafuta haya yanapotumika katika mitambo huwa na athari sana katika mazingira, kwa kuwa huongeza kiasi kikubwa sana cha hewa ya kaboni dayoksaidi katika anga na kuharibu utando wa ozoni. Matokeo yake ni kuwa kunakuwa na ongezeko la joto katika uso wa dunia, na ongezeko hili limeleta athari nyingi sana katika sehemu mbali mbali hapa duniani (nilishaliongelea hili katika mada zilizopita). hio ni moja, lakini pili ni kuwa iwapo kunatokea ajali majini na chombo kinachosafirisha mafuta kikahusika, mafuta hutapakaa katika maji (na kawaida mafuta huelea majini) na kuathiri viumbe wanaoishi katika maji. Kwa viumbe kama samaki, hushidwa kupumua kwa kuwa mafuta huzuia hewa kutoka na kuingia katika maji. Kwa ndege wanaoshi kwa kutegemea uvuvi, mara wapakaapo mafuta haya katika shughuli zao za uvuvi hushidwa kuruka kwa kuwa mbawa zao hushikamana na kukakamaa hivyo kwa wakati fulani hufa. Kwa sasa kuna mikakati kwa nchi zilizoendelea, kuachana na utegemezi wa nishati hii, lakini itachukua muda sana, ingawa inawezekena (rejea makala iliyopita).

MAJI
Kwa miaka mingi nguvu ya maji imekuwa ikitumika kwa namna mbali mbali. Kwa upande wa nishati, maji yamekuwa yakitumika moja kwa moja kuendesha mitambo ya kusagia nafaka, na kwa upande wa Tanzania bado mifumo hii inafanya kazi mpaka sasa. Kwa mfano, katika kijiji cha Kisiwani wilayani Muheza Mkoani Tanga, kuna mtambo wa kusagia nafaka ambao kuendeshwa kwa nguvu ya maji. Kwa upande wa pili, kutokana na maendeleo ya kiteknolojia, maji yanatumuka kuendeshea mitambo ya kuzalisha umeme, na kwa sasa dunia imekuwa tegemezi kwa nishati hii kwa kiasi kikubwa. Hli si shwari sana kwa upande wetu Tanzania, kutokana na maji kutokuwa ya kuaminika na kutokuwa na mfumo mzuri wa urejeshaji maji katika mabwawa mara baada ya kuyatumia. Pia hali ya hewa hasa suala la ukame limekuwa kikwazo kikubwa kwa uendelezaji wa nishati hii. Miradi mikubwa ya umeme wa nguvu ya maji si rafiki wa mazingira, kwa kuwa hutumia maeneo makubwa sana kuhifadhi maji, kwa hio kunakuwa na uhamishaji wa watu na wanyama na mara kadhaa husababisha mafuriko kwa watu waishio kando yake iwapo milango ya bwawa itafunguliwa kupisha matengenezo, kwa kuwa maji hufunguliwa kwa wingi sana. Pia miradi hii hutumia maji mengi sana, kwa hio viumbe wengine ambao hutegemea maji hayo mbele ya mabwawa hawapati maji kwa uhakika (kumbuka suala la vyura katika mradi wa umeme-Kihansi).

NYUKLIA
Ni moja ya nishati mbadala katika kupunguza tatizo la nishati. Kwa sasa ni nchi zilizoendelea tu ndizo zina uwezo na mamlaka ya kutumia nishati hii, kwa kuwa ni ghali sana. Pia inadhibitiwa sana na shirika na nguvu za nishati la Umoja wa Mataifa liitwalo 'International Atomic Energy Agency' (IAEA), kwa kuwa ni nishati hii hii itumikayo kutengeneza silaha za maangamizi, kwa hio wanahofia kuwa iwapo inaachwa bila ya udhibiti basi inaweza kutumika kwa malengo mengine, na si uzalishaji wa nishati. Kwa sasa nchi kama Japan, Korea Kaskazini, India, Iran*, Marekani, Norway na Urusi zinatumia nyuklia kwa kuzalishia nishati. Nyuklia huhitaji uangalizi wa hali ya juu sana, kwa kuwa ikivuja ina madhara sana kwa mwanadamu na viumbe wengine. Ajali ya kuvuja kwa mitambo ya nyuklia ilishawahi kutokea katika mji wa Chernobyl nchini Urusi mnamo mwaka 1986 na kusababisha madhara makubwa!
*(Vinu havijaanza kufanya kazi Iran)

UMEME WA MIONZI YA JUA
Ni teknolojia mpya kwa kiasi fulani, na ni rafiki wa mazingira. Ni mfumo wa kuvuna mionzi ya jua na kuzalisha umeme kwa kutumia mitambo maalum ijulikanayo kama 'Photovoltaics'. Uzalishaji wa umeme huu hutegemea sana uwepo wa mwanga wa jua na vihifadhi vya umeme huo kama betri. Umeme huu unafaa sana kwa mazingira yaliyo mbali na umeme wa gridi. Ni teknolojia ghali kwa kiasi fulani ingawa ni nzuri.

Kwa namna moja au nyingine tuendelee kujaribu kutafakari na kutafuta suluhisho la matatizo ya nishati yanayoikabili dunia, ili iwe mahali salama pa kuishi wanadamu.
Nafasi yako ni ipi katika hili?
Jadili!

10/11/06

MAFUTA MBADALA

UTANGULIZI
Kumekuwa na kilio sehemu mbali mbali duniani kuhusu uchafuzi wa hewa pamoja na athari zake ambazo dunia imeanza kuonja makali yake. Kilio hiki kinatokana na kuongezeka kwa kiwango cha moshi wenye sumu katika anga, na kuharibu mfumo mzima wa hali ya hewa. Athari zaidi zinaonekana katika utando wa 'ozone', ambao umetobolewa na hewa hizi za sumu. Kazi ya utando huu ni kuzuia mionzi ya jua yenye athari kutufikia moja kwa moja na kutuathiri. Athari ambazo dunia inazipata kwa sasa ni pamoja na ongezeko la joto duniani na kupungua kwa kiwango cha barafu katika milima, kupotea kwa baadhi ya jamii za mimea na wanyama kutokana na ongezeko hili la joto, ongezeko la magonjwa kama kansa na magonjwa mengine ya ngozi. Pia kuna maeneo ambapo utando wa moshi wa viwanda na magari ni mkubwa na hivyo husababisha mvua za tindikali. Mvua hizi hutokana na kuongezeka kwa hewa ya salpha dayoksaidi katika anga. Hewa hii ikizidi angani na kuchanganyikana na maji au unyevu hutengeneza tindikali ya salfarasi 'sulphorous acid', na hii ina madhara sana kwa mimea na wanyama. Tindikali hii huunguza majani ya mimea na kwa wanyama husababisha magonjwa ya ngozi. Kwa nchi za Ulaya ya Magharibi wanafahamu sana madhara ya mvua hizi za tindikali, kwani zimeharibu sana uoto wa asili. Kutokana na sababu hizi basi, kumekuwa na hatua mbali mbali za kupunguza hewa chafu katika anga, na moja ya hatua hizo ni kutumia mafuta mbadala ya kuendeshea mitambo badala ya mafuta ya jamii ya petroli.

MAFUTA MBADALA NI YAPI?
Msisitizo wa kutumia mafuta yasiyo na madhara sana kwa mazingira umekuwa ukipata kasi kadri siku zinavyosonga. Nchi zilizoendelea zimekuwa msitari wa mbele katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na uzalishaji mkubwa wa mafuta haya mbadala. Mafuta haya yanatokana na mimea kama mbono, miwa, michikichi, alizeti, maharage ya soya na mahindi. Kimsingi kila mmea una uwezo wa kutoa mafuta haya, kulingana na hali ya kiteknolojia iliyopo mahali husika. Mimea tajwa hapo juu, ukiacha miwa na mahindi, hutoa dizeli ambayo nchi zilizoendelea zinatumia kuendeshea mitambo ya namna mbalimbali. Miwa hutoa kimiminika kiitwacho 'ethanol' na hii kutumika sana kuendeshea mitambo pia. 'Ethanol' ni jamii ya pombe inayotengenezwa kwa njia ya mvukizo au mvuke. Kwa jina lingine rahisi hii ni 'gongo' ya kiwandani. Ni nyepesi sana na inashika moto haraka, hivyo wataalamu wameona inafaa kwa mitambo. Kumbuka kuwa karabai zinawashwa kwa mafuta ya jamii hii.

WAZALISHAJI WA MAFUTA MBADALA
Kwa upande wa 'ethanol', wazalishaji wakubwa kwa soko la dunia ni Brazili na Marekani na walianza karibu miaka ishirini iliyopita. Hawa wanazalisha bidhaa hii kutokana na makapi ya viwanda vya miwa. Pia nchi za umoja wa Ulaya ni wazalishaji wakubwa wa bidhaa hii. Kwa upande wa dizeli ya mimea, wazalishaji vinara ni Malaysia, China na Ujerumani. Malaysia ni mzalishaji wa kwanza wa mafuta ya mawese duniani, na dizeli wanayotengeneza inatokana na mawese. Wachina wanatengeneza 'ethanol' kutokana na mihogo na wanapata shehena kubwa ya mihogo hii kutoka Vietnam, Thailand na Indonesia.
Kwa upande wa Brazili, kuna magari milioni tatu yanayotumia ethanol! Wakati huo huo kuna magari milioni moja na laki tatu yanayotumia mchanganyiko wa petroli na ethanol.
(Chanzo cha takwimu: UNIDO/Berkeley BC Aprili 2006)

FAIDA ZA MAFUTA MBADALA
Mafuta haya hayatoi moshi wenye athari kwa anga, kwa kuwa hayana viambata vyenye sumu, kulinganisha na mafuta ya jamii ya petroli. Mafuta ya petroli huchanganywa na madini ya risasi 'lead' na hivyo yakitumika katika mitambo hutoa moshi wenye sumu katika anga.
Kwa kuwa mafuta mbadala hutokana na mimea, huongeza kipato kwa wakulima wa mazao yatoayo mafuta haya. Utengenezaji wa dizeli mbadala hauhitaji teknolojia za hali ya juu sana, tofauti na mafuta ya jamii ya petroli, hivyo hata nchi zinazoendelea zinaweza kumiliki mitambo ya kuzalishia mafuta haya.

TANZANIA NA MAFUTA MBADALA
Kumekuwa na tafiti mbalimbali zinazofanywa na watu na taasisi anuwai nchini Tanzania, kuhakikisha kuwa kunakuwa na maendeleo katika uzalishaji wa dizeli ya mimea. Baadhi ya taasisi zilizofanya utafiti wa mafuta haya ni pamoja na shirika la Msaada wa Kiufundi la Ujerumani (GTZ), Kampuni ya Kukuza Teknolojia (KAKUTE) ya Arusha na Taasisi ya Kuendeleza Nishati Endelevu na Mazingira Tanzania (TaTEDO). Kwa upande wa KAKUTE, wao wanafanya uzalishaji mdogo wa dizeli inayotokana na mbono, pamoja na kutengeneza sabuni zake.
Iwapo kutakuwa na msisitizo kwa watu binafsi, mashirika na serikali katika kuzalisha mafuta haya, basi tutaondokana na umasikini, kwa sababu bidhaa hii kwa sasa ina malipo mazuri katika soko la dunia. Nasema hivi kwa sababu tayarai nchini Tanzania tuna viwanda kadhaa vya miwa ambavyo hutoa makapi mengi ya kuweza kuzalisha ethanol na wakati huo huo mimea ya mbono husitawi hata katika maeneo yenye ukame.
Ni kitu kinachowezekana, ila inataka utashi!
Nafasi yako katika hili unaitumia kikamilifu?
Jadili!

9/20/06

YAJUE MALENGO YA MAENDELEO YA MILENIA

UTANGULIZI
Ni mara nyingi tumesikia, ama kuambiwa kuwa kuna malengo ya milenia, lakini huenda si wengi wetu tunaoyafahamu malengo hayo. Ni malengo yaliyoafikiwa mnamo Septemba 8 mwaka 2000, jijini New York Marekani na kuazimia kuwa ifikapo mwaka 2015, basi hayo maazimio waliyopanga yawe yametekelezwa kwa kiasi fulani cha kuridhisha, kama si kuyatekeleza kabisa.
Kwa ujumla kuna malengo manane ambapo nitayaeleza yote kwa ufupi katika makala hii na kuelezea lengo namba saba katika makala yake ya kujitegemea. Nitafanya hivi kwa sababu si busara kuelezea lengo namba saba pekee wakati malengo mengine hayafahamiki. Vile vile ni kwamba kufanikiwa kwa lengo moja basi ni njia ya mafanikio ya kuyafikia malengo mengine pia. Malengo haya yamewekewa viashiria, kujua kama yanatekelezeka ama la! Tafsiri kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili ni yangu!

YAFUATAYO NI MALENGO YA MAENDELEO YA MILENIA
1. Kupunguza Umasikini Uliokithiri pamoja na Njaa
Ndani ya lengo hili kuna malengo madogo mawili. Kwanza ni kupunguza hadi kufikia nusu, kwa kwa idadi ya watu ambao wanaishi kwa chini ya kiwango cha dola moja kwa siku, kati ya mwaka 1990 na 2015. (Kwa wakati huu, dola moja ya Kimarekani ni karibu sawa na shilingi 1200 za Kitanzania). Pili, ni kupunguza kwa zaidi ya nusu kwa idadi ya watu wasio na chakula.

2. Elimu Ya Msingi Kwa Wote
Kuhakikisha kuwa hadi mwaka 2015 mahali popote pale, watoto, kwa maana ya wasichana kwa wavulana wawe na uwezo wa kuhitimu elimu ya msingi.

3. Kukuza Usawa wa Kijinsia na Kuwawezesha Wanawake
Lengo ni kuondoa tofauti za kijinsia katika shule za msingi na sekondari hadi mwaka 2005 na katika nyanja zote kabla ya mwaka 2015.

4. Kupunguza Vifo Vya Watoto Wachanga
Lengo ni kupunguza kwa theluthi mbili, idadi ya vifo vya watoto walio katika umri wa hadi miaka mitano, kati ya mwaka 1990 na 2015.

5. Kuboresha Afya za Akina Mama
Lengo ni kupunguza kwa hadi robo tatu, idadi ya vifo vya wanawake wazazi, kati ya mwaka 1990 na 2015.

6. Kukabili Virusi Vya Ukimwi/Ukimwi na Magonjwa Mengine Makuu
Lengo la kwanza ni kupunguza na kuukabili Ukimwi na kubadili mwelekeo wake ifikapo mwaka 2015. Lengo la pili ni ni kukabili na kutokomeza malaria na magonjwa mengine makuu hadi kufikia mwaka 2015.

7. Kujihakikishia Uendelevu wa Mazingira
Hapa kuna malengo matatu madogo. Lengo la kwanza hapa ni kuingiza misingi ya maendeleo andelevu katika sera na mipango ya mataifa mbali mbali na kubadili mwelekeo na upotevu wa rasilimali. Lengo la pili ni kupunguza hadi nusu kwa idadi ya watu wasio na maji safi ya kunywa na huduma za maji taka. Lengo la tatu ni kuboresha makazi ya watu angalau milioni mia moja hadi kufikia mwaka 2020.

8. Kuanzisha Ushirikiano wa Kimaendeleo Duniani
Hapa kuna malengo mawili madogo. Kwanza, ni kujenga misingi ya utawala wa sheria na inayotabirika na isiyo na ubaguzi katika mifumo ya biashara na fedha. (Hii inahusisha pia kujifunga na misingi ya utawala bora, maendeleo na kupunguza umasikini, kitaifa na kimataifa). Pili, ni kuyapa kipaumbele mahitaji ya nchi masikini sana duniani (hii inahusisha kuondoa vikwazo katika masoko huru na usafirishaji wa bidhaa nje ya nchi. Pia kupunguza (ama kuondoa kabisa) madeni ya nchi hizi masikini na kutoa misaada kwa nchi ambazo zinaonyesha mwelekeo wa kuondoa umasikini).
Unaweza Kuyasoma zaidi Malengo hayo Hapa

Kwa hiyo ndugu msomaji wa makal hii, haya ndio malengo ya milenia yaliyoazimiwa mwaka 2000.
Katika makala ijayo, nitawaleteeni mjadala wa kiundani wa malengo kadhaa, tukianzia na lengo namba saba.

9/8/06

KIJANI, NJANO NA MAZINGIRA!

UTANGULIZI
Ndugu wasomaji wa blogu hii, leo naleta kwenu wazo jipya ama mjadala mpya. Kama kawaida yetu, ni jadi kuwa mtu akitoa wazo basi nasi tunapata wasaa wa kuchangia mawazo yetu, aidha kwa kuboresha ama kukosoa. Kwa hiyo basi, kwa leo nitaongelea rangi za kijani na njano, ambazo kwa siasa za nchi yetu si rangi ngeni hata kidogo, lakini leo ni siasa za kijani na njano katika upande wa mazingira.

MADA
Kwa wakereketwa wa siasa za nchi yetu, kijani na njano ni rangi za bendera ya chama tawala na pia ni mbili kati ya rangi nne za bendera ya taifa letu. Kwa ujumla rangi hizi kwa bendera zote mbili huwakilisha utajiri wa maliasili vikiwemo mimea, wanyama na madini yapatikanayo nchini mwetu. Huo ndio ufafanuzi uliowekwa yakini na serikali na chama kwa bendera hizo. Kwangu mimi, rangi hizi ni zaidi ya hapo, na humaanisha mambo mengine pia. Kwa wanachama wa chama tawala, wao huadhimisha kuzaliwa kwa chama chao kila mwaka tarehe tano mwezi wa pili. Aghalabu sherehe hizi huwa na shamra shamra nyingi zikiambatana na upokezi wa wanachama wapya na uzinduzi wa matawi mapya ya chama. Kwa mujibu wa takwimu rasmi, chama tawala nchini mwetu kina idadi ya wanachama rasmi wasiopungua milioni tano, nje ya mashabiki. Si haba, kwa nchi ya vyama zaidi ya kumi vya siasa na watu milioni thelathini na tano.
Kwa maana hiyo basi, nafikiri katika shamra shamra hizi wanachama hawa hupata wasaa wa kubadilishana mawazo na kuelimishana. Ni bora pia wakaelimishana maana ya rangi za bendera za chama chao kama hawajaelezwa, hasa kwa wanachama wapya. Pia, ni bora wakaelimishwa matumizi sahihi ya rangi hizo.

WAZO
Iwapo kila mwaka katika tarehe tajwa hapo juu wanachama wangekumbushwa (au kuelimishwa?) namna ya kutunza ukijani popote pale walipo, basi katika suala zima la mazingira tungekuwa mbali sana. Hebu chukua mfano, kila mwanachama kati ya hawa milioni tano (acha mashabiki) alazimike kupanda miti miwili tu mahali panapostahili, katika kumaanisha ukijani wa bendera ya chama chake, basi kwa mwaka tunakuwa na miti milioni kumi! Si suala dogo wala porojo, na hii ni kwa siku moja tu kwa mwaka mzima. Ukichanganya na miti tunayopanda kila Januari, basi tungekuwa tunasikia kwa mbali sana suala la ukame na kukauka kwa vyanzo vya maji.
Lakini, hata si kwa kupanda miti, basi iwe ni kuokota taka na kuzihifadhi mahali panapostahili ili kutunza ukijani, nadhani bustani nyingi sana mijini zingekuwa kijani sana hadi sasa, badala ya kuzungushia uzio kila mahali penye bustani ili watu wasikanyage bustani zetu. Ni suala la elimu na utashi tu.

Kwani haiwezekani?
Jadili

8/31/06

TUJIFUNZE TOKA KWAO

UTANGULIZI
Mu hali gani wasomaji wa blogu hii?
Kama nilivyodokeza siku zilizopita, nipo kaskazini mwa dunia yetu, hususan nchini Norway. Kwa ujumla muda huu ndio majira ya joto yanamalizika kwa huku, muda si mrefu tutakabiliana na baridi na barafu.

HALI YA HEWA
Kwa kawaida, hapa mahali naambiwa na wenyeji kuwa mvua haina msimu maalum, inanyesha wakati wowote (nafikiri ni kwa sababu ya misitu mingi) na kuwa karibu na bahari. Kwa kawaida wakati wa baridi joto hushuka hadi nyuzi -28 hadi -32 kulingana na maeneo. Na kuna wakati fulani (kama sasa) jua linazama muda wa saa 2.30 hadi saa 3.30 usiku kwa saa za hapa. Na kuna maeneo ya kaskazini mwa nchi ambapo jua huwa halizami kabisa kwa baadhi ya miezi, kwa hiyo ni suala la kuangalia saa tu katika kufanya mambo yako. Kwa mfano, wakati nasafiri kwa ndege toka Uholanzi kwenda Oslo, ilikuwa saa 4 kasoro usiku na jua lilikuwa likiwaka!

UTUNZAJI WA MAZINGIRA
Nchi hii ina watu milioni 5 tu na nadhani robo ya hawa ni wahamiaji, kwa hiyo maeneo mengi ni misitu na nyumba chache sana. Kwa maana hii basi, basi wengi hujazana katika miji mikubwa kama Oslo, Trondheim, Stavanger na Bergen, kwa hiyo uharibifu wa mazingira si kwa kiasi kikubwa. Hali kadhalika, nishati kubwa zitumikazo huku ni mafuta na umeme, ingawa kuni hutumika mara chache sana kwa ajili ya kuzalisha joto katika baadhi ya nyumba wakati wa majira ya baridi. Hata hivyo wengi hutumia mitambo ya kuzalisha joto itumiayo umeme. Ukataji miti upo, hasa miti ya kupandwa, kwa ajili ya kuzalisha mbao na bidhaa nyingine za namna hiyo, na ukiwa katika jiji hili utakutana na magari mengi tu ambayo yanapakia magogo kupeleka viwandani. Kwa ujumla, hawa watu wamedhibiti vumbi kwa kiasi kikubwa wakisaidiwa na hali ya hewa (mvua za mara kwa mara na misitu), tofauti na kwetu ambapo kuna vumbi kila karibu kila mahali. Kwa hapo Tanzania, naweza kufananisha mitaa ya huku na ile ya jiji la Dar es Salaam kama vile barabara ya Haile Selasie, Garden, Shaaban Robert na Magogoni, kwa maana ya kwamba njia zote zina lami, mpaka njia za waenda kwa miguu.
Kuna udhibiti mkubwa wa vyombo vya majini, hasa kuhusu umwagaji wa mafuta na taka nyingine. Kwa watu niliowahoji, wanasema kuwa kuna adhabu kali sana iwapo mtu atakutwa anatupa taka majini, kwa kuwa kuna maeneo mengi sana hapa mahali ya kukusanyia taka. Hata hivyo taka hizi hutengwa kulingana na aina zake, kwa maana ya kwamba, kunakuwa na mapipa kama matatu katika eneo moja. Haya hukusanya taka za namna mbalimbali kila pipa peke yake, yaani kuna pipa la makopo ya maji na bia, pipa la masalia ya vyakula na pipa la taka ngumu kama za plastiki. Pamoja na udhibiti huo bado kuna wavunja sheria vile vile, ambao hutupa taka mahali popote watakapo na hawajali lolote.

USAFIRI
Kuna mpangilio mzuri sana wa njia za usafiri hapa mahali, na hakuna misururu kama ile ya jiji kubwa hapo nyumbani. Kwa mfano, nyakati za asubuhi kunakuwa na treni katika njia (reli) zaidi ya kumi katika stesheni kuu ambazo husafirisha abiria kwenda miji mbali mbali katika kazi na nyingi ya hizi hupita chini ya ardhi kwa baadhi ya maeneo. Kila baada ya dakika zisizozidi 7 treni hutoka stesheni kuu kwenda mahali fulani. Kwa mfano, mimi naishi Oslo na nafanya kazi mji wa Lysaker, inanichukua dakika kama kumi na tatu tu kufika kazini, umbali kama wa kilometa 30 hivi. Hali kadhalika kuna treni zinazopita katikati ya jiji katika mitaa mbali mbali, hizi zenyewe ni kwamba, reli zake zimepitishwa katikati ya lami, kwa hiyo magari na treni huchangia njia. Hizi ni nyingi kuliko nilizotaja hapo juu. Hali kadhalika kuna mabasi mengi sana makubwa katikati ya jiji, yanayosafirisha watu kutoka na kuingia jijini Oslo. Naweza kusema hizi ndio dala dala za huku. Pamoja na uwingi huu, ukichanganya na magari binafsi hakuna misururu!

KWA NINI HAKUNA MISURURU?
Kwanza, mpangilio wa mji ni mzuri sana, kuna njia nyingi sana kwa hiyo haimlazimu mtu kupita njia moja na kuna njia nyingi ambazo hupita juu ya nyingine (fly overs) kama lilivyo daraja la Manzese, na kati ya hizi kuna nyingine ni ndefu kwa kilometa kadhaa. Hali kadhalika kuna barabara zipitazo katika mahandaki, nazo ni nyingi pia.
Pili, jiji la Oslo ni kwa ajili hasa ya makazi na ofisi chache muhimu. Kwa maana hiyo basi, viwanda vingi vipo nje ya jiji hili, ambapo huwalazimu wafanyakazi kusafiri toka jijini hapa kwenda nje ya jiji kikazi, kwa hiyo basi huu ni mfumo wa kwenda na kurudi (two way), tofauti na nyumbani, ambapo asubuhi na jioni misururu huwa ya namna moja (mara nyingi) hasa wakati wa kwenda na kurudi kazini.
Tatu, kuna kundi kubwa la watu ambao hutumia baiskeli kwenda kufanya kazi zao ndani na nje ya jiji. Na kusema kweli baiskeli ni nyingi mno hapa mahali (kama Tanga au Morogoro vile) hadi zinakuwa kero. Nafikiri ni nyingi kutokana na utambarare wa jiji na hali ya hewa ya baridi, kwa hiyo mtu hachoki sana. Hizi nazo husaidia sana kupunguza misururu barabarani (nilishawahi kuongelea suala hili katika baadhi ya makala zangu zilizopita).
Kuna mengi sana ya kuongelea lakini kwa leo naishia hapa.
Nitaendelea kutafiti mambo mengine zaidi na kuwajulisha.

Wao wameweza wana nini? Na sisi tushindwe kwa nini? Kuna nini katikati hapa?
Jadili.

8/17/06

NIKO UPANDE WA PILI WA KIJIJI CHETU



Mu hali gani wana blogu wenzangu?
Mimi mzima kabisa na kwa sasa nablogu tokea upande wa pili wa dunia, ambayo tunasema kuwa sasa ni kama kijiji. Sasa basi, mimi nipo upande wa kaskazini wa kijiji chetu (dunia). Nipo jijini Oslo nchini Norway. Nitaendelea kublogu tu hata huku, pamoja na kwamba majukumu ni mengi kazini. Nitawagawia kile nitakachojifunza huku bila choyo.

7/12/06

MFUMO IKOLOJIA NI NINI?

Utangulizi
Kwa maelezo rahisi, mfumo ikolojia ni namna ya maisha katika eneo fulani ambapo viumbe wa aina mbali mbali ikiwa ni pamoja na wanyama na mimea hutegemeana, aidha kwa chakula ama hifadhi au vyote kwa pamoja. Mfumo huu wa maisha hushirikisha viumbe wote waliopo katika eneo husika, kuanzia wale wakubwa wanaoonekana kwa macho hadi wale tusioweza kuwaona kwa macho. Mmoja wa wanasayansi wanzilishi wa nadharia hii ni mwanasayansi wa Uingereza Bwana Arthur Tansley (1871- 1955). Yeye ni kati ya watu ambao walifanya kazi kubwa sana ya utaifi katika kuweka utambuzi wa mifumo ikolojia. Tuchukue mfano wa kitu kama dimbwi la maji. Katika dimbwi, kunaweza kuwa na viumbe hai wa namna mbali mbali waliopo pale kama vile vyura, viluwiluwi, mbu, utando wa mwani, bakteria na viumbe wanaofanana na hao. Katika mfumo kama huu, unaweza kukuta kuwa viluwiluwi hula mwani, na vyura hula mbu wanaotafuta maeneo ya kutagia mayai katika dimbwi husika. Mbu nao huhitaji hifadhi katika dimbwi kwa mazalio yao. Ni kwa namna hii basi tunaona kuwa kunakuwa na kutegemeana kwa viumbe hai hawa, ikiwa wote hutaji dimbwi hili kwa namna mbali mbali. Jitihada zozote za mwanadamu katika kuliharibu dimbwi hili, ni kuharibu mfumo mzina na mustakabali wa viumbe hai waliopo pale.
Tupate mfano mwingine wa mfumo ikolojia. Tuchukue mfano wa msitu mdogo au kichaka. Katika kichaka kunaweza kuwa na viumbe kama panya, nyoka, bakteria, mimea mikubwa na midogo, mashimo, wadudu wa namna mbali mbali pamoja na minyoo. Katika mazingira kama haya, kwa namna moja au nyingine viumbe hai hawa watategemeana, aidha kwa hifadhi au chakula, au vyote. Kuondolewa kwa kiumbe kimoja katika mfumo huo no kuhatarisha mustakabali wa viumbe wengine ambao hutegemea kuendesha maisha yao kutokana na kiumbe huyo. Mfano, katika kichaka, kuondolewa kwa panya kunaweza kuwa na athari kwa nyoka ambao hutegemea panya kama chakula chao, Koundolewa kwa mimea kunaweza kuathiri wadudu ambao hutegemea mimea hio kwa hifadhi na lishe.

FAIDA ZA MFUMO IKOLOJIA
Kama tulivyoona katika mifano hiyo hapo juu, kuna uhusiano mkubwa sana kati ya kiumbe na kiumbe. Kutoweka kwa kiumbe mmoja kunaweza kuwa na athari kwa viumbe waliosalia katika mfumo huo. Katika mfumo huu mwanadamu hajasahaulika, na ndio chanzo kikuu cha athari zilizo nyingi katika mifumo ikolojia.

Faida
Husaidia uwepo wa viumbe mahali mbali mbali. Mfano nyuki huchavusha maua katika kujitafutia chakula chake (chavua) na hivyo hufanya maua yasitawi vizuri. Maua haya huzaa matunda ambayo ni chakula cha viumbe wengine ambao ni pamoja na wanadamu. Kwa hivyo basi, bila nyuki na jamii nyingine za wadudu kama vipepeo,hatuwezi kuwa na uchavushaji. Mfano mwingine, mimea hupumua hewa ya oksijeni ambayo ni muhimu sana kwa maisha ya wanyama, na hali kadhalika wanyama hupumua hewa ya kaboni dayoksaidi ambayo husaidia uhai wa mimea. Kwa hivyo basi, bila mimea wanyama hawana maisha, na bila wanyama mimea haiwezi kuishi. Ni katika mazingira haya basi kuna utegemeano wa viumbe hai, kwa hiyo kutoweka kwa kiumbe hai kimoja kunaweza kuwa na athari kwa viumbe hai wengine ambao kwa namna moja au nyingine hutegemea uwepo wa kiumbe hicho. Kuna mifano mingi sana ya kutegemeana kwa viumbe hai, ambapo nafasi hii haitoshi kuelezea kila kitu, isipokuwa tu tuelewe kuwa viumbe hai wanategemeana sana kwa kila hali.

WAJIBU WETU
Ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa tunalinda viumbe hai kwa kila hali, ili tusiweze nasi kuathirika, kwani wao wakiathirika nasi twaathirika pia.

Je unachukua hatua gani kuhakikisha viumbe hai wanaokutegemea wanaishi salama?
Jadili...

6/28/06

UNAFAHAMU WALINZI HAI WA MAZINGIRA?

U hali gani msomaji wa blogu hii.
Katika mada ya leo, nataka kukufahamisha kitu muhimu sana katika suala zima la athari za uharibifu wa mazingira, na mustakabali wake katika viumbe hai. Nataka kuongelea kitu kinachitwa bioindicators. Mimi naita viashiria, (nitashukuru kama nitapata tafsiri ya kiswahili sanifu ya jina hilo)

UTANGULIZI
Hiki ni Kitu gani?
Hizi ni jamii za mimea au wanyama (wanyama ni pamoja na wadudu) ambazo huashiria uharibifu mazingira ya sehemu fulani, katika uso wa dunia. Viumbe hawa, huwa katika mfumo-ikolojia wa eneo fulani. Iwapo kunakuwa na mabadiliko katika hali ya mazingira ya mahali walipo, ambayo si ya kawaida, basi viumbe hawa huonyesha mabadiliko fulani, aidha katika mfumo wao wa lishe, maumbo, kibiolojia au wa kitabia. Kila kiumbe kina aina yake ya tahadhari ya uharibifu huu wa mazingira, iwe ni mimea au wanyama.

KAZI ZA VIUMBE HAO (BIOINDICATORS)
Viumbe hai hao wana kazi kubwa kadhaa katika suala zima la ulinzi wa mazingira. Kwanza, hutoa utambuzi wa uharibifu wa mazingira katika eneo fulani walipo. Pili, hutoa taarifa za uvamizi wa kitu ambacho si cha kawaida katika eneo husika kutokana na uharibifu ambao unatokea. Tatu, hutoa taarifa juu ya hali ya usafi wa mazingira wa eneo husika na nne, hutumika kufanya majaribio ya hali ya usafi wa maji, kama yamechafuliwa au la.

VIASHIRIA-MIMEA (PLANT INDICATORS)
Katika utafiti makini wa kisayansi, kuwepo au kutokuwepo kwa jamii fulani ya mimea katika maeneo fulani, huweza kutoa taarifa muhimu sana juu ya athari za kimazingira zinazotokea katika eneo hilo. Tuchukulie mfano wa mimea fulani midogo sana ya kijani "lichens", inayoota kama utando katika miamba na miti yenye unyevu nyevu . Hii mara nyingi hupatikana katika misitu. Mimea hii huweza kubadilika haraka sana iwapo kuna mabadiliko yasiyo ya kawaida katika msitu, kama vile mabadiliko ya hali ya hewa, ukame na mfumo wa hali ya hewa ya msitu husika. Kutokomea kwa mimea hii katika eneo husika inaweza kuwa ni kiashiria cha hali tete ya uharibifu wa kimazingira kama vile uwingi wa hewa ya naitrojeni, madini ya oksaidi ya salfa au vichafuzi vingine vya jamii ya salfa.

VIASHIRIA-WANYAMA (ANIMAL INDICATORS)
Viumbe hai wadogo wadogo, wasioonekana kwa macho, huweza kuwa viashiria vya athari za mazingira, iwe ni katika maji au nchi kavu. Viumbe hawa wana uwezo wa kuzalisha protini mpya katika miili yao, ili kujikinga na athari mbaya za uharibifu wa mazingira, iwapo kunakuwa na vitu visivyo vya kawaida vinavyochafua mazingira yao. Protini hizi, huweza kuwa ni dalili za tahadhari, kuwa kuna uharibifu fulani katika mazingira walipo viumbe hao. Wanyama wengine hubadili matabaka ya miili yao, ili kujilinda na athari hizi. Hivyo basi, wataalamu wanapoona mabadiliko yasiyo ya kawaida katika maisha ya wanyama hawa, huweza kutambua uharibifu uliopo katika mazingira ya eneo husika na kuchukua hatua.

MATUMIZI YA VIASHIRIA HIVI
Kama tulivyoona hapo juu, viumbe hai viashiria hubadilika hali zao kunapokuwepo na mabadiliko katika mazingira walipo. Hata hivyo mabadiliko haya hutofautiana kati ya viumbe hawa. Mifumo hii ya kijenetiki, hutumika sana katika kutunza maliasili, kwa kujua mabadiliko katika hali za viumbe hai katika misitu. Ni rahisi kwa kiasi fulani kujua mabadiliko katika mifumo-ikolojia ya maeneo fulani kwa kutumia viumbe hawa. Uchafuzi wa maji pia huweza kugundulika kwa kutumia viumbe hai hawa, hasa kunapokuwa na madini kama 'cadmium au benzene' katika maji. Iwapo kunakuwa na madini haya katika maji, miili ya viumbe hai viashiria huwa na mabadiliko yasiyo ya kawaida. Madini haya si salama kwa matumizi ya binadamu.

Vyura, pia ni kati ya viumbe hai ambao hutumika mara kwa mara na wanasayansi katika kugundua athari za uharibifu wa mazingira. (kama una kumbukumbu nzuri, utakumbuka suala la vyura wa Kihansi Morogoro, walipoathirika kwa kukosa kiasi fulani cha maji ambacho ni muhimu kwa maisha yao, baada ya mradi wa umeme kutumia maji mengi kuliko kawaida). Kuna sababu kadhaa za mabadiliko ya maisha ya vyura, hasa kunapokuwa na uharibifu wa mazingira yao kwa namna fulani. Vyura hutaga mayai katika maji, hivyo muda wao mwingi huutumia katika maji. Hutaga mayai yaliyo wazi (nje) hivyo hutegemea maji kuyaangua. Wana ngozi ambayo kwa kiasi fulani hupitisha maji, hivyo huweza kuhisi mabadiliko mara moja. Ilishatokea pia katika Ziwa Manyara mkoani Manyara, kuwa kulikuwa na mabadiliko katika mtiririko wa maji. Mimea jamii ya mwani (algae) iliathirika, na ndege jamii ya korongo na heroe ambao hutegemea mimea hiyo kwa lishe yao pia waliathirika. Hii ni mifano michache tu, lakini kuna viumbe wa namna nyingi ambao hutumika kugundua athari za mazingira kwa maeneo mbali mbali hapa duniani.

TUFANYE NINI?
Hatuna budi kuangalia kwa makini shughuli zetu, ambazo nyingi ya hizo si rafiki wa mazingira, kama vile uchomaji wa misitu, uchimbaji na usafishaji wa madini kwa kutumia kemikali zenye athari kwa mazingira. Ni vizuri tukazalisha, lakini pia ni vema kuangalia mustakabali wetu na viumbe wengine ili tusiwaathiri na tusijiathiri sisi wenyewe. Viumbe hai viashiria, ni watoa taarifa wazuri wa athari tunazofanya, hivyo tuangalaie upya namna nzuri ya kutumia rasilimali zetu.

6/15/06

SERIKALI NA MIFUKO YA PLASTIKI "RAMBO"

UTANGULIZI
Hivi karibuni, yaani tarehe 15 Juni 2006, waziri wa fedha mheshimiwa Zakhia Hamdani Meghji aliwasilisha bajeti ya matumizi ya serikali kwa mwaka wa fedha wa 2006/2007 katika kikao cha bajeti cha bunge la Tanzania. Kama ilivyo kawaida, wengi wetu tulihamishia usikivu wetu Dodoma kusikiliza yale tuliyoandaliwa kwa mwaka wa fedha ujao. Kwa mtazamo wa wengi ni kwamba bajeti hii ina afadhali ukilinganisha na iliyopita, kwa kuwa imekumbuka maeneo mengi muhimu, kama vile kupunguza kodi katika mafuta, kuongeza ruzuku kwa pembejeo za kilimo na kuongeza mishahara ya watumishi. Ni mengi yanavutia katika bajeti ya mwaka huu, lakini kama ilivyo ada watu tunatofautiana katika mawazo. Kuna wanaopinga kuwa bajeti haijafanya lolote katika kumuinua mtu wa kipato cha chini. Maneno haya tumeyasikia mahali pengi hasa kutoka kwa wanasiasa maarufu, lakini ni haki yao kusema hivyo, kwani katiba inamruhusu kila mtu kutoa maoni yake kadri anavyotaka.
Kwa upande wangu, nilivutiwa na kipemgele cha kuongeza kodi katika mifuko laini ya plastiki, maarufu kama 'rambo' kutoka 15% hadi 120%, naunga mkono kodi hii, na ndio suala ambalo nimeliweka katika mjadala moto hapa mahali.


AINA ZA MIFUKO YA RAMBO
Mifuko ya rambo hutengenezwa kwa plastiki laini aina ya Low Density Polyethylene (LDP). Kuna mingine ambayo hutengenezwa kwa plastiki ngumu aina ya High Density Polyethylene (HDP), lakini hii si maarufu sana kama ile laini. Tofauti rahisi ya aina hizi za mifuko ni kwamba, mifuko laini haipigi kelele inapopapaswa na ile migumu hupiga kelele. Hii ndio tofauti rahisi na ya wazi ambayo mtu wa kawaida hutumia kutofautisha aina hizi. Lakini hata katika mfumo wa kikemikali, bidhaa zitumikazo kutengenezea aina hizi za mifuko hutofautiana. Tofauti hii ni kwamba, malighafi itumikayo kutengenezea mifuko laini haiwezi kurejeshwa katika hali yake ya awali kwa sababu wakati wa utengtenezaji wake, hufanyika badiliko la kikemia (chemical Change) badala ya badiliko la kiumbo (physical change) ambalo ni rahisi kugeuza na kutengeneza kitu kingine.

MATUMIZI
Ingawa kwa kiasi kikubwa matumizi hufanana, kuna tofauti ndogo ndogo. Mara nyingi mifuko laini ni midogo kwa muundo na myepesi, kwa hio haitumiki kubeba vitu vizito, tofauti na ile migumu ambayo hutumika kubebea vitu vizito. Kwa mfano, mara nyingi, watunza bustani za miti hutumia mifuko migumu katika kuotesha miti kwa kuwa hudumu kwa muda mrefu tofauti na ile laini ambayo huharibika ndani ya muda mfupi. Kuna matumizi ya aina mbali mbali ya mifuko hii kadri mtu atakavyotaka, na niliyotaja hapo juu ni baadhi tu.

ADHA ZA MIFUKO HII
Mifuko ya rambo imekuwa ikipigiwa kelele sana sehemu mbali mbali kuwa inachafua mazingira, kutokana na utaratibu wetu mbovu wa utupaji wa taka. Mifuko hii hupatikana kwa bei rahisi sana, na wakati mwingine hutolewa bure kabisa baada ya mtu kununua bidhaa. Mara nyingi mifuko hii huzagaa mahali pengi kutokana na kutoitupa katika mahali stahili. Suala hili limekuwa sugu, kwa nafikiri ndio sababu imeamua kupandisha kodi yake kutoka asilimia 15 hadi 120! (rejea Bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2006/07 ukurasa wa 45). Hali kadhalika, mifuko hii mara nyingi hutumika kubebea vyakula kwa hiyo huwa na masalia ya vyakula wakati fulani. Ndege wa jamii mbali mbali, hasa jamii ya kunguru huiokota na kuisambaza kila mahali, katika harakati zao za kujitafutia riziki, kiasi cha kuleta kero. Vivyo hivyo, wakati wa mvua mifuko hii hukusanyika pamoja na taka nyingine na kuziba mitaro ya kupitisha maji taka. Hali hii husababisha maji kutuamac na kuleta harufu mbaya. Maji haya ni mazalio mazuri ya mbu waletao malaria. Ni maji haya haya ambayo yanaleta kipindupindu kisichoisha katika baadhi ya miji yetu. Mifuko hii imesambaa sana katika barabara zote kuu na kuchafua maeneo ya kando ya barabara hizo, hasa ziendazo mikoani. Hii ni kutokana na baadhi ya mabasi yasafirishayo abiria kutokuwa na utaratibu wa ukusanyaji wa taka katika mabasi yao, ili ziweze kutupwa mahali stahili. Mifuko hii, haiozi kirahisi ifukiwapo, hivyo husababisha usumbufu mara eneo husika linapotumiwa kwa matumizi mengine.

UTATUZI WA ADHA HIZI
Kuna namna nyingi sana endelevu za kuweza kukabiliana na suala zima la uchafuzi wa mazingira hasa suala la kutupa taka ovyo. Kwanza, inabidi tuwabane wasafirishaji wa abiria hasa wa masafa marefu, ambao kwa namna moja au nyingine hulazimika kusimama njiani ili kupata chakula. Hawa ndio chanzo kikuu cha kusambaa kwa mifuko laini njiani. Nasema hivi kwa sababu, muda wa dakika kumi hadi kumi na tano wanazotoa kwa ajili mapumziko na chakula hazitoshi, hivyo abiria hulazimika kunuua chakula na kula ndani ya gari na kutupa mifuko laini njiani, mara baada ya kumaliza kula. Tuwabane ili wawe na sehemu za kuhifadhia taka katika mabasi yao. Suala hili linawzekana, na linafanya kazi. Kama huamini, tembelea mbuga ya wanyama ya Mikumi, uone walivyo wakali kuhusu kutupa mifuko na na chupa za maji katika maeneo yao.
Suala lingine, ni kutoa elimu ya uhifadhi wa mazingira, hasa kwa watu wa mijini kuhusu namna ya kutupa taka ngumu mahali panapotakiwa. Inashangaza sana kuona kuwa watu hutupa mifuko laini na taka nyingine ngumu chini au pembeni ya pipa la taka wakati pipa liko hapo hapo. Hawa wanahitaji kuelimishwa kama si kuadhibiwa.

MIFUKO MBADALA
Pamoja na serikali kuchukua hatua katika kudhibiti usambaaji wa mifuko laini, kuna kundi kubwa la watu ambao wameona kuwa serikali haijawatendea haki kabisa. Baadhi yao ni wafanyabiashara waagizao mifuko hii toka nje ya nchi, na wasambazaji wao waliopo mahali mbali mbali hapa nchini. hata hivyo ningependa kutoa ushauri kwao, na kwa wengine. Ushauri huu ni kuwa, tuanze kutumia mifuko mbadala ambayo ni rafiki wa mazingira. Kwanza tutumie mapakacha. hii ni mifuko ya asili inayotengenezwa kwa makuti (majani ya minazi na michikichi). hufaa sana kubebea bidhaa za namna anuwai kama vile matunda, nazi viazi na kadhalika. ikifukiwa, mifuko hii huoza na kusababisha mbolea. Pili, tutumie bidhaa zinazotengenezwa kwa ukindu na mimea ya jamii yake. Hufaa saa kwa matumizi ya namna mbali mbali na tukiitumia tutakuwa tunakuza uchumi wa nchi kwa kuwaongezea kipato watengenezaji wake. tatu, tutumie mifuko ya karatasi za kawaida kama vile mifuko ya khaki. Mifuko ya namna hii huoza mara inapofukiwa (biodegradable), hivyo haiathiri mazingira. Pia kuna mifuko inayotengenezwa kwa nyuzi za 'Jute'. Jute ni malighafi itumikayo kutengeneza magunia. Mifuko hii ya jute ilikuwa maarufu sana siku za nyuma, kabla ya ujio wa rambo na ilikuwa na msaada mkubwa sana. Kwa sasa imeanza kurudi sokoni, kwa hiyo hatuna budi kuitumia kwa wingi. Kuna mifuko ya namna nyingi ambayo inaweza kutumika badala ya mifuko laini ya plastiki, ni suala la uamuzi na utashi tu.
Inawezekana kufanya mabadiliko. Je uko tayari?
Jadili.

6/13/06

UNG'OAJI WA MIANZI MKOANI IRINGA: NI SAHIHI?



UTANGULIZI
Ndugu wanablogu wenzangu, nimesoma makala ya Bw Johnson Mbwambo ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha Waandishi wa Habari za mazingira Tanzania, ambayo ilitoka katika gazeti la Nipashe tarehe saba mwezi Juni. Ilinivutia na kunishitua kidogo, lakini nikaona niisome na kutoa maoni yangu kuhusu utaratibu mzima wa Serikali ya Mkoa wa Iringa kuhusu mpango wa kung'oa mianzi katika vyanzo vya maji. Yeye Bw Mbwambo ameandika makala kutokana na mahojiano aliyofanya na viongozi wa Mkoa wa Iringa juu ya uamuzi wa serikali na NGO katika mkoa wa Iringa, wa kutaka mimea jamii ya mianzi iliyo katika vyanzo vya maji ing'olewe, kwa kuwa si rafiki wa mazingira, kwa maana ya kwamba inakausha vyanzo vya maji. Ningependa kuongelea masuala machache muhimu katika makala yake hiyo isemayo "Operesheni ya kung'oa mianzi yapamba moto mkoani Iringa" .

MIANZI NI NINI?
Hii ni jamii ya mimea ambayo wataalamu wa elimu-mimea wameiweka katika kundi la majani yanayotoa maua, na si miti. Hii inatokana na jamii nyingi za mianzi kuwa na sifa za majani zaidi kuliko miti. Mianzi hupatikana duniani kote, lakini hutofautina kutokana na tofauti ya hali ya hewa ya sehemu mbali mbali. Mianzi ya kitropiki ni tofauti na ile ya nchi za baridi, hivyo hivyo mianzi ya sehemu kame ni tofauti na mianzi ya sehemu zenye unyevu wa kutosha. Mimea hii hupatikana katika jamii ya Bambuseae. kuna jamii 91 na aina zaidi ya elfu moja za mianzi kote duniani na kila aina ina sifa tofauti kulingana na mahali aina hiyo ilipo.Jamii za mianzi hutofautiana kwa urefu, kuna ile ambayo ikikua sana hufikia sentimeta chache hadi kukomaa, na ile ambayo hukua hadi kufikia urefu wa meta arobaini hadi kukomaa. Upana wa shina la muanzi hupishana sana kati ya jamii na jamii kutoka milimita moja hadi thelathini. Hata utoaji wa maua wa mianzi hutofautiana sana. Kuna jamii ambazo hutoa maua baada ya miaka 28 tu na ile ambayo hutoa maua baada ya miaka 120, (rejea Troup 1921) Synchronous'Gregarious' Flowering Species Table. Kuna jamii nyingi za mianzi ambazo hukua kwa wastani wa sentimeta 30 kwa siku (futi moja!), na baadhi ya jamii nyingine zimewekwa katika rekodi kwa kukua kwa wastani wa sentimeta 100 (mita moja!)kwa siku.
Kwa hapa Tanzania, mianzi hupatikana katika mikoa mingi sana,kama vile Tanga, Mbeya, Iringa, Ruvuma na Rukwa na kadhalika na matumizi yake pia hutofautiana kati ya mkoa na mkoa.


MATUMIZI YA MIANZI
Aina za matumizi hutofautiana kati ya sehemu na sehemu, na kati ya jamii moja na nyingine. Kwa wenzetu Wachina mianzi michanga huliwa na ile iliyokomaa hutumika kutengenezea karatasi, na vile vile hutumika katika matambiko yao kwa kuombea umri mrefu wa kuishi. Kwa Wahindi, mianzi ni alama ya urafiki wa heshima, kwa maana kwamba mtu kukirimiwa kwa bidhaa za mianzi (kama viti, vikombe nk) humaanisha urafiki. Mianzi hutumika kutengezea vyombo vya ndani, kama vile vikombe, nyungo, vikapu na matenga. Kwa Wanyakyusa na Wasafwa wa mkoani Mbeya, kuna vifaa vya kukamulia na kuhifadhia maziwa ambavyo huita 'kitana' au 'tana'.Mianzi hutumika kutengenezea viti, vitanda na meza, mianzi hutengeza madaraja, hujenga nyumba ambazo husilibwa kwa matope pamoja na vyoo. Mianzi hutumika kutengeneza mikongojo (fimbo za kutembelea) na bakora, hutumika kutengenezea mitumbwi pamoja na sakafu. Kuna jamii ambazo hutengeneza filimbi za mianzi (zipo katika mikoa ya Morogoro, Mbeya, Iringa na Rukwa). Mianzi hupandwa sehemu za makazi kama uzio.
Kwa ujumla kuna matumizi mengi mno ya mianzi, ambayo si rahisi kuyaeleza yote hapa.
Kibiolojia, mianzi ina faida yake pia. Husaidia kuzalisha hewa ya oksijeni, ambayo ni muhimu kwa maisha ya wanyama.

Mkoani Iringa mianzi ina matumizi ya aina yake. Kwanza mianzi michanga hutumika kutengenezea pombe maarufu ya 'Ulanzi' ambayo husafirishwa hadi mikoa jirani ya Ruvuma na Mbeya. Mianzi hii michanga hukatwa inapofikia kimo cha kuanzia futi mbili hadi nne na hapo huwekwa kifaa maalum chenye uwazi kwa juu kilichotengezwa kwa mwanzi pia. Kifaa hiki hugema utomvu wote toka katika mwanzi mchanga na kuuhifadhi> Utomvu huu baadaye huchachuka na kuwa pombe-ulanzi. Ni pombe maarufu sana makoani hapo. Pili, mkoa wa Iringa ni maarufu kwa ulimaji wa nyanya. Mianzi hutumika kutengenezea matenga ya kuhifadhia na kusafirishia nyanya kwenda sokoni.Tatu, mianzi hutumika kutengeneza mazizi ya mifugo, hasa maeneo ya vijijini, pia ni bidhaa muhimu sana ya ujenzi wa nyumba, hii ni sehemu zote, yaani mijini na vijijini.

MGONGANO WA MASLAHI
Amri ya serikali ya mkoa wa Iringa kwa upande fulani inaweza kuwa sahihi, hasa kama kuna ushahidi wa kutosha wa kuweza kutumika kuhalalisha uondoaji wa jamii hii ya mimea katika vyanzo vya maji. Sina uhakika kama amri hii inatekelezwa mkoani Iringa pekee au na maeneo mengine yenye mianzi katika vyanzo vya maji. Tukumbuke kuwa, miaka michache iliyopita kulikuwa na mjadala kuhusu miti jamii ya eucalyptus, kwamba ukuaji wake huhitaji maji mengi, hivyo jamii hii ya mimea ilikuwa hatari kwa vyanzo vya maji. Uondoaji wa miti hii ulileta migingano katika maeneo mengi ya nchi, hasa ikizingatiwa kuwa ni miti tegemeo kwa sekta nyingi sana, hasa viwanda. Miti hii (eucalyptus)ni nishati kuu katika mashamba na viwanda vya chai vilivyopo nchini, na pia ni tegemeo kwa TANESCO kwa kuwa hutengeneza nguzo za kusambazia umeme kwa kutumia miti hii. Miti hii ni nishati tegemeo katika kukausha tumbaku. Ni kwa sababu hizi na nyingine, ambazo zilifanya amri kwa watu, ya kuondoa miti hii iwe na malalamiko kutoka kila upande.
Ni ukweli kuwa mianzi mingi imepandwa katika sehemu zenye maji (ikiwa ni pamoja na vyanzo vya maji, kwa kuona kwangu mashamba mengi ya mianzi katika mikoa ya Iringa na Mbeya. Sijapata uhakika kama kweli mimea hii hukausha vyanzo vya maji, ndio sababu nasisitiza kuwa ni vizuri kukawa na ushahidi wa kutosha usio na mawaa kama vile machapisho ya kitaalamu, kabla ya 'kuisulubu' mimea hii muhimu. Kwa upande wa wadau ambao hutegemea sehemu ya mapato yao kutokana na mianzi(kama vile wagema na watengeneza matenga),inawezekana wakawa na mwitikio hasi, hasa kama hawajaelimishwa vya kutosha kuhusu athari za mianzi katika vyanzo vya maji. Hawa wataona moja kwa moja kuwa ajira yao inayoyoma.
Kwa upande wa serikali, wao ni watekelezaji wa sera zilizotungwa na bunge, ambazo aghalabu huwa za manufaa kwa jamii kwa ujumla. Hivyo basi, si ajabu kwa serikali kutekeleza sera ambayo inaonekana kuwa ina manufaa kwa wananchi wake. Kwa mtazamo huo, kama serikali imeona kuwa mianzi haifai kuwa katika vyanzo vya maji, basi haina budi kuiondoa mimea hiyo katika maeneo ya vyanzo vya maji ili kuwanusuru wananchi wake na baa la ukame (kama lililotokea miezi michache iliyopita).

UPANDAJI MITI MBADALA
Katika makala ya Bw Mbwambo, serikali imetaja na kupendekeza aina kadhaa za miti ambazo zitapandwa katika maeneo ya vyanzo vya maji na sehemu nyingine ambazo mianzi itaondolewa.Miti hiyo ni migunga, mizambarau na mivinje. Kuna jamii nyingine za miti ya asili ambazo zipo mkoani Iringa na zinafaa kupandwa katika vyanzo vya maji. Jamii hizi ni mikuyu (sycamore/fig tree) "ficus sycomorus", mivumo "ficus sur" ,albizia gummifera, mikoche "hyphaene compressa" na mingine mingi. Hii inafaa sana katika ulinzi wa vyanzo vya maji.

MUHIMU
Kama kweli serikali imepania kuondoa mianzi katika vyanzo vya maji, basi ni bora wananchi wakaelimishwa kuilinda miti mbadala, ili isije ikahujumiwa na wale walioondolewa mianzi yao, hili lipo na laweza kutokea.

Ndugu msomaji wa makala hii, ni nani yu sahihi katika suala hili? Ni serikali, au ni wananchi walioishi na mianzi hii kwa muda mrefu?
Jadili

6/12/06

ASILI, FAIDA NA ADHA ZA MAGUGU-MAJI

UTANGULIZI
Magugumaji ni kati ya mimea inayosifika sana kwa kuzaliana hapa duniani, inayopatikana katika mazingira yenye maji kwa msimu wote, kama vile kwenye mito, ziwani,kwenye madimbwi, kwenye mitaro na miferejini.Unaweza kuvuna tani mia mbili za magugumaji kwa ekari moja tu! Ni mmea wa kijani ambao humea kwa kutambaa, hutoa maua ya rangi ya zambarau au hudhurungi na huweza kurefuka hadi kimo cha futi tatu. Mmea huu ni moja ya mimea ya jamii ya "Pickerelweed" au "pontederiaceae" (jamii ya magugu yanayostawi katika maji). Kwa jina la kitaalamu, mmea huu hufahamika kama 'eichhornia crassipes' na kwa Kiingereza hujulikana kama 'Water Hyacinth'.

ASILI YA MAGUGUMAJI
Takwimu za wataalamu wa elimu-mimea, zinaonyesha kuwa asili ya mmea huu ni katika nchi za kitropiki za Amerika ya Kusini, lakini kwa sasa mmea huu umesambaa katika mabara yote. Kwa nchi kama Marekani mmea huu ulisambaa kati ya mwaka 1884 na 1885 mjini Louisiana. Kuna mtu ambaye alikuwa katika mnada wa pamba katika nchi za Amerika ya kusini, akachukua mmea huu kama pambo la nyumba yake. Kwa kutojua, alitupa masalia ya mmea huo katika mto wa Mtakatifu Jones,baada ya kuzaliana sana kuliko alivyotarajia, na hatimaye mmea huo ukasambaa katika majimbo mengine ya Marekani. Kwa Afrika Mashariki, inasadikika kuwa mmea huu uliletwa enzi za ukoloni wa Waingereza, yaani kuanzia mwaka 1920, na hupatikana sana katika Ziwa Viktoria katika Mikoa ya Mara na Mwanza kwa upande wa Tanzania, na maeneo mengine yanayozunguka ziwa hili katika nchi za Kenya na Uganda.

MAZINGIRA YAKE
Magugumaji hustawi sana katika maji yaliyotuama, au yale yenye mwendo mdogo sana. Kama nilivyotaja hapo mwanzo, mmea huu hupatikana ziwani, mitoni, madimbwini, mitaroni na maeneo mengine oevu yanayofanana na hayo. Huweza kuota kwa kutawanya mbegu zake au kwa vikonyo vyake, na hutengeneza chakula chake moja kwa moja toka katika maji.

FAIDA NA MATUMIZI YA MAGUGUMAJI
Mmea huu una faida kadhaa, na huweza kutumika kwa shughuli mbali mbali za kiuchumi. Mmea huu, kama nilivyotaja hapo juu, hupata chakula chake kutokana katika maji, hivyo basi, hutumika kuchuja maji taka na kuwa maji masafi kwa matumizi ya kubinadamu yasiyo ya moja kwa moja, kama vile kilimo cha umwagiliaji na ujenzi. Mfano mzuri unapatikana katika madimbwi ya maji taka ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo maji taka hukusanywa katika eneo moja na kuchujwa katika hatua mbali mbali kabla ya kusafishwa kwa matete na magugumaji, katika hatua za mwisho. Maji haya hutumika kumwagilia mpunga na mboga mboga, na pia hutumiwa na wanyama pori walio katika eneo hilo. Faida nyingine ya magugumaji ni katika kazi za sanaa za mikono. Nchini Kenya kwa mfano, kuna mradi ujulikanao kama 'Water Hyacinth Utilization Project' (WHUP), katika mwambao wa ziwa Viktoria, ambao hufanya matumizi endelevu ya magugu maji. Mradi huu hushughulika na utengenezaji wa vikapu, majamvi, kofia, meza, vivuli/viambaza, makaratasi, vitabu, karata, mikeka na vitu vingine muhimu kwa kutumia sehemu anuwai za mmea huu, kama vile maua, majani, shina na vikonyo. Kwa mfumo huu basi, mmea huu umesababisha ajira kwa watu wa maeneo hayo.
Ajira nyingine ya namna yake, ni kwa wale walioajiriwa katika udhibiti wa usambaaji wa magugu haya. Hawa huajiriwa ili kudhibiti magugumaji kusambaa ndani zaidi ya ziwa, kama tutakavyoona hapa chini.

ADHA ZA MAGUGUMAJI
Katika maeneo mengi duniani ambapo magugumaji hupatikana, mara nyingi huchukuliwa kama mmea usiotakiwa, ha hivyo kila juhudi hufanywa kuhakikisha kuwa mmea huu unaondoshwa. Shida kubwa ni kwamba, mmea huu huzaliana kwa kasi kubwa ya ajabu, kiasi kwamba juhudi kubwa pamoja na gharama huhitajika ili kudhibiti usambaaji huu wa kasi. Kama tulivyoona hapo mwanzo kuwa mmea huu hustawi katika mazingira yenye maji, basi mmea huu ni adha kwa shughuli zote ambazo hufanyika katika maji. Mmea huu huzuia shughuli za uvuvi, hunasa katika panga boi za vyombo vya majini,huzuia uzamiaji na upigaji mbizi, huziba mabomba ya kusafirishia maji ya kuzalishia umeme na shida nyingine nyingi. Magugumaji husababisha utando mkubwa mfano wa jamvi katika maji, na kuzuia mionzi ya jua na hewa ya oksijeni kupenya chini ya maji, hivyo huzuia upatikanaji wa viumbehai wengine katika eneo hilo, hasa jamii ya mimea. Mazingira haya ya ukosefu wa oksijeni katika maji, yakichangiwa na utando mkubwa wa magugumaji hufanya maji yasitembee na hivyo kuwa mazalio makuu ya mbu waletao malaria. Ni sababu hizi hufanya watu wengi wayachukue magugumaji na kuchukua hatua za kuyatokomeza. Kuna kukinzana kwa kiasi kikubwa kwa mawazo katika suala zima la magugumaji.
Hapa ni kila mtu na mtazamo wake, watengenezaji wa samani huona yana faida, na watumiaji wengine wa maji huona kama ni bughudha tu!

UDHIBITI NA UTATUZI WA ADHA ZA MAGUGUMAJI
Kuna taasisi kadhaa ambazo hushughulika na udhibti wa ueneaji wa magugumaji. Pia kuna watu binafsi ambao hukerwa na maimea hii, hivyo huamua kuondoa kwa mikono. Kwa upande wa ziwa Viktoria, nchi zote tatu za Afrika Mashariki zina mipango endelevu ya kudhibiti kuenea kwa magugumaji, na kwa Tanzania na mradi wa LVEMP (Lake Victoria Environmental Management Project), ambao pamoja na mambo mengine hushughulika na usafi na ulinzi wa mazngira wa ziwa tajwa. Katika nchi nyingine zenye magugumaji, kuna wadudu wajulikanao kwa kitaalamu kama 'neochetina' ambao 'hupandwa' makusudi ili kula magugumaji. Hata hivyo, kiwango kikubwa cha kuzaliana cha magugumaji huzidi uwezo wa wadudu hao wa kuyala. Inasemekana pia kuwa samaki aina ya sangara ambao hupatikana kwa wingi katika ziwa Viktoria walipandikizwa kwa ajili ya kula magugumaji, lakini kasi yao ya ulaji inazidiwa kwa mbali na kasi ya ukuaji wa magugumaji. Kuna dawa za viwandani za kuulia mmea huu, lakini haishauriwi sana kuzitumia kwa kuwa nyingi kati ya dawa hizo si rafiki wa mazingira, na huua viumbe wengine waishio majini.Badala yake, mitambo ya kusaga magugumaji hutumika zaidi, hasa katika ufukwe wa ziwa hili kwa upande wa Kenya.

Ndugu msomaji wa makala hii, umeona faida na adha za magugumaji,japo kwa ufupi tu. Una mtazamo gani kuhusu mmea huu?
Jadili

6/6/06

YAJUE MAENEO YA RAMSAR KATIKA TANZANIA (RAMSAR SITES)

Utangulizi
Maeneo ya Ramsar ni sehemu ya ardhi oevu duniani, (wetlands) ambayo yana umuhimu wa pekee duniani katika suala zima la uhifadhi wa mazingira. Ardhi oevu ni ile ardhi ambayo kwa msimu wote wa mwaka huwa na unyevunyevu. Jina hili "Ramsar" linatokana na mji wa Ramsar nchini Iran ambapo ndipo mkataba wa kutunza maeneo ya ardhi oevu duniani ulisainiwa, mnamo mwaka 1971. Kwa hiyo basi, mwaka 1971 ndipo yalipofanyika maamuzi ya kulinda maeneo ya ardhi oevu dhidi ya uharibifu, ili yaweze kutumika katika shughuli endelevu, kama vile vyanzo vya maji. Mpaka sasa, kuna mataifa 152 duniani yaliyotia sahihi mkataba huu wa kulinda ardhi oevu, ikiwemo Tanzania. Kuna maeneo tengefu 1608 ya Ramsar duniani yanayochukua ukubwa wa hekta milioni 140, kati ya haya Tanzania tuna maeneo manne tu, ambayo tutayaelezea hapa chini.


Nini umuhimu wa Maeneo haya?
Maeneo ya Ramsar yana umuhimu wa kipekee katika jamii. Kwanza, yana bioanuwai adimu sana hapa duniani ambazo aghalabu hupatikana maeneo hayo tu. Pili, ni vyanzo vikuu vya maji katika maeneo mengi diniani, hivyo, kama yakiharibiwa kwa shughuli za kibinadamu basi uhai wa viumbe hao adimu utatokomea pia. Maeneo haya ni chanzo kukuu cha nishati ya umeme, ambapo kwa namna moja au nyingine, mito inayozalisha umeme hutiririka kutoka katika nyingi ya ardhi hizi oevu. Chukulia mfano wa bonde la mto Rufiji, bonde hili huanzia katika milima ya Uporoto mkoani Mbeya na kusambaa katika mikoa mingine ya Iringa na Morogoro, ambapo kuna bonde la mto Kilombero ambalo ni maarufu kwa kilimo cha mpunga na ni moja ya maeneo tengefu ya Ramsar. Kwa mfano huu mmoja, nadhani tunaweza kuelewa japo si kwa undani, juu ya maeneo haya muhimu.

Maeneo Ya Ramsar Tanzania ni yapi?
Tanzania tuna maeneo manne tengefu, yaliyo chini ya mkataba wa Ramsar. Maeneo haya ni ardhi oevu ya Muyovozi katika mto Malagarasi-Kigoma (13/04/2000), ardhi oevu ya bonde la Ziwa Natron-Manyara (04/07/2001), bonde la mto Kilombero-Morogoro (25/04/2002) na bonde la Rufiji-Mafia hadi Kilwa-Pwani (29/10/2004). Katika mabano ni tarehe ambazo maeneo hayo yaliingizwa katika orodha ya maeneo tengefu ya Ramsar. Kwa hiyo, maeneo haya yanalindwa na mikataba ya kimataifa, ambapo hairuhusiwi kufanya shughuli zozote za kiuchumi kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi, uwindaji na ukataji miti.

Ni Sifa zipi zinatakiwa, ili Eneo liwe chini ya Mkataba wa Ramsar?
Kuna sifa kuu tisa zinazofanya eneo likubalike kuwa katika uhifadhi wa mkataba wa Ramsar. Sifa hizi zimegawanywa katika makundi manne tofauti, kwa hapa nitazichangaya zote.

1. Inatakiwa eneo oevu husika liwe na umuhimu wa kimataifa kwa kuonesha bioanuwai ambazo ni wakilishi, za kipekee, zisizopatikana mahali pengine popote ila hapo tu, iwe ni mazingira ya asili au ambayo hayajaribiwa uasili wake na liwe eneo ambalo liko katika sehemu stahili ya kijografia.

2. Eneo litahesabiwa kuwa na umuhimu wa kimataifa iwapo lina viumbe adimu ambao wapo katika hatari ya kutoweka kabisa toka katika uso wa dunia kutokana na muingiliano wa viumbe hai.

3. Ili eneo husika lihesabike kuwa na umuhimu w kimataifa, inatakiwa liwe lina viumbe hai (mimea na wanyama) ambavyo ni muhimu kwa ajili ya kuendeleza uanuwai wa kibiolijia (uasili)wa eneo husika.

4. Eneo litahesabiwa kuwa na umuhimu w kimataifa iwapo linasaidia upotevu/uwepo wa mimea/wanyama katika mzunguko mzima wa maisha ya viumbe hao (life cyles), au eneo ambalo linatoa ulinzi hao dhidi ya uharibifu, katika mazingira mbali mbali.

5. Iwapo eneo linatunza jamii ya ndege 20,000 kwa kawaida kwa wakati mmoja, basi hili litahesabiwa kuwa katika orodha ya maeneo tengefu.

6. Iwapo eneo linahifadhi asilimia moja ya aina za ndege kutoka jamii mbalimbali za ndege hao, litahesabiwa kuwa katika orodha hii.

7. Iwapo eneo lina hifadhi kiasi kikubwa cha jamii ya samaki wa asili (si wa kupandwa kama sangara wa Ziwa Viktoria) historia ya maisha ya samaki hao, mwingiliano wa jamii za samaki hao, ambao ni wakilishi wa eneo hilo oevu na ambaohangia utajiri wa bioanuwai duniani, litaignizwa katika orodha ya maeneo ya Ramsar.

8. Iwapo eneo ni chanzo kikuu cha chakula walacho samaki, sehemu ya kutagia/kuzaliana samaki, sehemu ya kupita ya samaki kwa ajili ya kutafuta mazalio au chakula, ambapo samaki hupategemea kwa maisha yao, basi eneo hilo litaingizwa katika orodha tajwa hapo juu.

9.Sifa hii inafanana sana na namba 6 hapo juu, lakini hii inahusika na wanyama kwa ujumla wake.

Kwa hiyo, ili eneo liwe katika orodha ya Ramsar, halina budi kuwa na moja kati ya sifa zilizoainishwa hapo juu, ingawa inatokea mara nyingine eneo moja kuwa na sifa kadhaa kati ya hizo.
Kwa sababu hizi basi, ilikuwa ni lazima kwa serikali kuwaondoa wafugaji katika ardhi oevu za Kilombero (Morogoro) na Mbeya) kutokana si tu na umuhimu wa kitaifa, bali kimataifa pia. Wafugaji na wakulima hawana budi kuelimishwa juu ya umuhimu wa maeneo oevu kwa maisha ya binadamu, badala ya kuyaharibu kwa kulima na kufugia makundi makubwa ya wanyama katika maeneo haya nyeti. Ni kwa sababu hizi ambapo serikali iliamua

6/5/06

SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI...TUNAJIFUNZA NINI?

Kila mwaka, tarehe tano Juni ni siku ya mazingira duniani. Watu katika nchi mbali mbali hapa ulimwenguni huadhimisha siku hii kwa namna mbali mbali, wengi aghalabu hufanya shughuli mbali mbali za utunzaji wa mazingira. Kwa hapa kwetu nchini, sherehe hizi huambatana na kufanya kazi za utunzaji mazingira, kama vile uokotaji wa taka mahali mbali mbali, upandaji wa miti sehemu za wazi na kadhalika. Lakini kwa upande mwingine, hapa nchini kwetu upandaji wa ,miti kitaifa hufanyika kila mwaka siku ya Januari mosi, yaani siku ya mwaka mpya. Nadhani hii tarehe imewekwa makusudi kwa sababu kwa maeneo mengi (kama si yote) hapa nchini huwa ni msimu wa mvua. Kwa hio, ili miti iliyopandwa iote vizuri, ni lazima ipate maji ya kutosha, kutokana na mvua hizi.

Ni kwa nini basi tunaadhimisha siku hii?
Nitaanza kwa kufafanua maana ya dhana hii ya "mazingira" . Mazingira, kwa ujumla wake, ni vitu vyote ambavyo humzunguka mwanadamu. Vitu hivi ni kama maji, miti, milima, mabonde, miamba na kadhalika. Tunaadhimisha siku hii kwa sababu nyingi. Sababu kubwa ni kwamba, bila mazingira, mwanadamu hawezi kuishi. Kwa hiyo mwanadamu hana budi kuboresha mazingira yake ili aendelee kuishi. Mwanadamu akiharibu mazingira, basi anaharibu uhai wake mwenyewe.
Kila mwaka kunakuwa na semina na makongamano sehemu anuwai hapa duniani, kwa ajili ya kujadili suala hili la mazingira kwa mapana yake, lengo kubwa ikiwa ni kuyaboresha. Mmoja wa mikutano hii maarufu ni ule uliofanyika katika mji wa Kyoto nchini Japan tarehe 11 Desemba mwaka 1997. Mkutano huu ulitengeneza mkataba wa kupunguza uchafuzi wa mazingirana ulianza kufanya kazi tarehe 16 Februari 2005, ambapo ulilenga kupunguza ongezeko la joto duniani, ambao ulifikia maamuzi magumu ya kupunguza uharibifu wa anga kwa kupunguza gesi zenye sumu kutoka viwandani. Mpango (mkataba) huu hufanya kazi kupitia chombo kijulikanacho kama "United Nations Framework Convention on Climate Change" (UNFCCC). Kumbuka kuwa Marekani haikutia sahihi mkataba huu, kwa kuogopa kuua viwanda vyake, ambavyo huzalisha gesi nyingi sana za sumu duniani. Chombo hiki ndicho hutoa mwongozo wa kiwango cha gesi za sumu zinazotakiwa kutolewa kutoka viwandani ili kutoharibu "ozone" ambayo ni kiwambo cha gesi ambacho huzuia mionzi ya jua yenye madhara kutufikia moja kwa moja toka angani. Mpaka sasa, nchi 163 zimeweka sahihi katika mkataba huu.
Mkutano huu wa Kyoto ulitanguliwa na ule wa tarehe 5 Juni mwaka 1992 katika mji wa Rio de Janeiro nchini Brazil, ambao nao malengo yake yalikuwa ni kupunguza uharibifu wa mazingira na kutunza bio anuwai.

Hali ya mazingira ikoje hapa kwetu?
Hali ya mazingira yetu kwa ujumla ni mbaya, kwamba tunashindwa kuyatunza kwa kwa usahihi. Ni suala la kawaida kwa watu mbali mbali kulima na kujenga katika vyanzo vya maji, mbuga za wanyama na hifadhi za taifa. Ni kawaida kwa wenye viwanda kumwaga taka zenye sumu katika mito na vijito, na mifano hai ipo mingi tu. Ni kawaida kutupa ovyo chupa za maji tukishakunywa maji, na ni kawaida kujisaidia haja ndogo mahali palipoandikwa "USIKOJOE HAPA". Ni kawaida kwa watu kutupa taka chini pamoja na kwamba mahali hapo pameandikwa 'TUPA TAKA HAPA". Kwa nini? Kwa faida ya nani?Hatumkomoi mtu, ila ni sisi wenyewe tunajisababishia vifo vinavyoweza kuepukika kabisa. Tunapotiririsha maji ya sumu ya viwandani katika mito, ilhali tunavua samaki katika mito hiyo hiyo tunatarajia nini? Tunakatazwa kutumia zebaki katika kusafishia madini lakini hatuachi, kwa nini? Tunaharibu vyanzo vya maji na mito inakauka, tunakosa maji na umeme, hatuoni kuwa tunajinyima haki? Kwa nini? Ni viwanda vingapi vinachafua hali ya hewa kwa gesi za sumu? Hatuvifahamu viwanda hivi? Tumechukua hatua gani?
Je tunachukua hatua madhubuti katika utunzaji na uhifadhi wa mazingira?
Jadili
Soma makala maalum ya siku ya mazingira hapa

HII INAWEZEKANA-TUWE NA UTASHI WA KISIASA!

Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na misururu mirefu ya msongamano wa magari hasa katika jiji la Makamba (Dar es Salaam). Hii inatokana na ongezeko kubwa la watu pamoja na magari, lisiloendana na rasilmali za kuweza kuhimili ongezeko hili. Kwa maana hii basi, uwezo wa barabara zetu (carrying capacity), wa kuhimili tatizo hili ni mdogo sana. Na aghalabu misururu hii ipo katikati ya jiji na katika barabara zote kubwa za jiji hili. Hali hii inasababisha usumbufu kwa wananchi, hasa suala la kuchelewa kazini, kwa kutumia muda mrefu kusafiri umbali mfupi. Wagonjwa wa dharura mara nyingine hufia njiani kwa sababu ya kucheleweshewa matibabu kutokana na misururu hii. Ni suala la kawaida kukuta mtu anatoka kwake muda wa saa 12 asubuhi na kufika kazini kama saa 2.30 hivi, uchelewevu wote huu ukisababishwa na msongamano wa magari. Kumekuwa na midahalo mbalimbali katika vyombo vya habari, vyombo vya usafiri na katika vijiwe sehemu kadha wa kadha kuhusu adha hii, lakini sina uhakika kama midahalo hii inawafikia warasimu, ambao wanatakiwa kutatua tatizo hili. Ni kero kubwa kwa jiji hili, ingawa hatujaona nia thabiti ya wakubwa wa nchi hii ya kulidhibiti tatizo hili. Kuna nadharia kadhaa, ambazo zikifanyiwa kazi na na kuwekwa katika vitendo na warasimu zinaweza kabisa kupunguza, kama si kumaliza tatizo hili katika nchi hii.

1. Mipango Miji
Suala la kujaza ofisi zote katikati ya jiji, kwa mtazamo wangu naona si sahihi sana. Kwa mfano, asilimia kubwa ya wizara zote zipo Dar es salaam, tena katikati ya jiji, ukiachilia mbali wizara ya Mifugo na Tawala za mikoa na serikali za mitaa, ambazo zipo Dodoma. Sasa basi, wananchi ambao huwa na shida anuwai, hulazimika kujazana katika wizara hizi ili kutatuliwa shida zao. Sasa katika hali kama hii unafikiri misururu katikati ya jiji itaepukikaje? Suala hili laweza kutatuliwa kwa kuwa na majengo mengi nje ya jiji. Majengo kama Ubungo Plaza na Millennium Towers pale Kijitonyama yalistahili kujengwa mengi na iwe ni nje ya jiji, maeneo kama Mbezi, Kibamba, Boko, Bunju na Tegeta ili kupunguza msongamanao wa watu na magari. Kwa maana hii basi, kungekuwa na kupishana, kwamba mtu anaishi Magomeni na anafanya kazi Bunju na mwingine anaishi Kariakoo na kufanya kazi Mbagala, hivyo misururu isiyo ya lazima isingekuwepo jijini. Lakini kwa sasa hali ni kinyume chake, maghorofa mengi marefu hujengwa katikati ya jiji. Suala hili huongeza idadi ya ofisi na na watu na kufanya katikati ya jiji kuwa na watu wengi. Tujaribu kutumia nadhari hiyo, inawezekana kabisa kupunguza tatizo.

2. Uhamishaji wa miji mikuu
Suala hili liliwahi kufanyiwa kazi na Hayati Mwalimu Julius Nyerere, kwa kuanzisha mradi wa kuweka Makao makuu ya nchi pale mkoani Dodoma yaani Capital Development Authority (CDA). Sina uhakika na sababu zilizofanya mradi huu usiendelee kwa kasi, lakini kwa wataalam wa mipango miji wanajua ni nini Mwalimu alidhamiria kukifanya. Lengo la mradi kama huu, aghalabu huwa ni kupunguza msongamano usio wa lazima katika baadhi ya miji, kwa kusambaza huduma katka mikoa mbalimbali. Kuna baadhi ya nchi zimefanikiwa kutekeleza mipango kama hii. Nijeria ilihamisha makao makuu yake kutoka Lagos kwenda Abuja, Ivory Coast inahamishia makao yake makuu kutoka Abidjan kwenda Yamoussokrou na kadhalika. Hii inasaidia sana katika kupunguza misongamano isiyo ya lazima katika miji mikuu.
Nafikiri ni kwa sababu hii ambapo Mahakama Kuu na Benki Kuu za hapa kwetu zina kanda kadhaa katika mikoa mbali mbali. Lengo ni kupunguza misongamano na safari zisizo za lazima jijini Dar es Salaam.

3. Upandaji wa Pikipiki na Basikeli
Kuna haja ya kuwa na mipango endelevu ya kupanda pikipiki na basikeli kwa wingi, ili kupunguza uwingi wa safari za magari. hili linawezekana kama wananchi tutaamua kwa moyo mmoja kupanda basikeli kwa sehemu ambazo makazi yetu hayapo mbali na ofisi zetu. Kwa mfano unakuta mtu anaishi Mwenge Dar, na anafanya kazi Makumbusho au pale Sayansi. Huyu nae analazimika kukaa katika msururu wa magari na kuchelewa kazini ilhali kama angekuwa na basikeli, ingemchukua muda mfupi sana kufika ofisini kwake. Kuna ulazima wa kuwa na fikira mbadala katika suala zima la kupunguza msongamano usio wa lazima. Suala hihi la pikipiki na basikeli liende sambamba na kutembea, kwa maana kwamba kama mtu anaona sehemu yake ya kujipatia riziki haiko mbali na makazi yake basi ni bora akatembea ili kuepuka adha ya msongamano. Inawezekana!

4. Udhibiti wa Watu kukimbilia Mijini
Suala hili kwa kiasi kikubwa husababishwa na watu waliopo vijijini kukuta hawana huduma muhimu za jamii, na hivyo hujikuta hukimbilia mijini kutafuta huduma hizi kwa namna yoyote. Utoro huu ni mkubwa sana hasa kwa vijana, ambao huamua kukimbilia mijini baada ya kuhitimu masomo yao, kwa hisia kuwa mjini kuna kila kitu, kwa hiyo 'hakiharibiki kitu'. Ni kwa mtazamo huu wa vijana wa vijijini ambapo hujikuta wamejazana mijini na kukosa ajira na kuongeza msongamano usio wa lazima. Hii hufanya tuanze kunyang'anyana rasilmali chache zilizopo mijini, ikiwemo usafiri na makazi.
Utatuzi wa tatizo hili unawezekana iwapo tu warasimu watilia mkazo utekelezaji wa mahitaji muhimu ya watu wa vijijini kama vile shule bora, huduma za afya na maji.

Kwa ujumla, adha zilizoainishwa hapo juu zinaweza kutatuliwa iwapo tu kutakuwa na utashi wa kisiasa wa wananchi na serikali kwa ujumla katika kuzivalia njuga adha hizo. Masual haya yanawezekana na rasilmali za utekelezaji wake tunazo, wakiwamo watu, suala ni utashi wa kisiasa tu. Inawezekana!

5/26/06

JE UNAITHAMINI NA KUIPENDA TAALUMA YAKO?

U hali gani mpenzi msomaji wa blogu hii?
Ningependa kuongelea suala muhimu sana katika maisha yetu ya uanazuoni. Mwaka jana Desemba 30, 2005 wakati rais wetu anahutubia bunge la Jamhuri ya Muungano (wa Tanzania?) kwa mara ya kwanza, aligusia kwa uchungu sana suala la wanataaluma kutotumia ipasavyo taaluma yao, lakini yeye aliita "Kutukanisha Taaluma" Katika mfano mmojawapo, aliwatuhumu Mabwana (nafikiri na Mabibi) ardhi kuwa wanauza maeneo ya wazi yaliyotengwa kwa ajili ya michezo, ili yatumike kwa shughuli za ujenzi, wakati taaluma yao hairuhusu kufanya hivyo.
Ukiliangalia suala hili kwa undani, utaona ukweli wake, hasa ukifuatilia suala la migogoro ya ardhi katika Tanzania, wilaya ya Kinondoni ikiongoza. Inasemekana kuwa hakuna wilaya yenye migogoro mingi ya ardhi katika Jiji la Dar es salaam kama Kinondoni. Zingatia kuwa karibu asilimia kubwa ya nyumba za bei mbaya kwa jiji hili ziko kinondoni ukianzia na Mbezi beach, Masaki, Oysterbay, Kinondoni nk. Hili la watu wa ardhi ni kundi moja la 'watukanisha taaluma'.
Kundi jingine alilogusia Mheshimiwa Rais ni la wanasheria, ambao hujigamba kwa kujiita "Learned Brothers/Sisters". Hawa nao hawajambo kwa kusaini mikataba ya ajabu ajabu ambayo ni wengi wetu tunaifahamu na inatukera. Ni hawa hawa waliosaidia kupitisha kwa kishindo sheria ya takrima, ambayo, kwa sasa wanataaluma wasiokubali kutukanisha taaluma yao wamesema kuwa haifai. Hebu tujiulize, iweje msomi wa shahada kadhaa za sheria akatia sahihi ya kuipitisha sheria ambayo anajua (au hajui?) kuwa inakiuka katiba ya nchi? Utajiitaje msomi ikiwa huthamini elimu na maadili ya taaluma yako?
Kuna kundi jingine la wanataaluma wanaotukanisha taaluma yao. Hawa ni wale ambao waliruhusu ujenzi wa majengo marefu sana pale Jijini Dar, hasa Kariakoo bila majengo hayo kukidhi viwango vya kitaalamu vinavyotakiwa. Matokeo ya kutukanisha taaluma yao tunayaona sasa, ambapo majengo kadhaa yameamriwa kubomolewa, kwa kuwa hayakidhi viwango sahihi vya ujenzi. Ina maana kuwa kabla ya majengo haya kujengwa hayakukaguliwa kama yanakidhi viwango vinavyotakiwa? Hivi hawa nao wanaithamini taaluma yao?
Hivi, ni viwanda vingapi hapa Tanzania ambavyo vinazingatia usalama wa mazingira kwa kushughulikia taka zizalishwazo na viwanda hivi? Wataalamu wa Tathmini za Athari za Mazingira (EIA) mpo? Mnatumia taaluma yenu kama ipaswavyo? Mmeona rangi ya maji ya mto Kizinga pale Mbagala Mission? Na rangi ya mto Kiwira pale Ilima Rungwe ikoje? Mmechukua hatua gani?
Kuna mambo mengi sana ya kuongela kuhusu uhusika wetu katika taaluma zetu, lakini hasa tujiulize, ni kwa nini baadhi yetu 'tunatukanisha' taaluma zetu? Mpaka hapo, ni kwa nini vyeti vya elimu ya hawa watukanishaji taaluma isitiliwe mashaka? Je hayo ni matokeo ya "kudesa?" au kuzunguka mbuyu?
Ni kwa kiasi gani tunathamini taaluma zetu?
Jadili

5/22/06

UKO HURU KUNENA!

Karibu katika blogu hii. Hapa tutakuwa tukijadili mada mbali mbali pamoja na kutoa maoni katika mada husika.
Zingatia kuwa Katiba ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 (toleo la 1998) sura ya kwanza sehemu ta tatu, ukurasa wa 23 ibara ya (18) (1) kinachohusu uhuru wa mtu kutoa mawazo yake , kinatamka bayana kuwa 'bila kwenda kinyume cha sheria za nchi, kila mtu ana haki na uhuru wa kutoa mawazo/fikra zake, na kutafuta, kupokea na kusambaza taarifa au fikra kwa kutumia njia yeyote ile, bila kujali mipaka ya nchi na ana haki ya ya kutoingiliwa katika mawasiliano au mpashano huu wa habari'. (2) 'Kila raia ana haki ya kupashwa habari muda wote kuhusu matukio mbali mbali katika nchi na dunia kwa ujumla wake, ambayo ni muhimu kwa watu na maisha yao na muhimu kwa jamii nzima pia.'
Hivyo basi, ni kwa kutumia uhuru huu ambapo blogu hii inafanya kazi , na ndugu msomaji/mchangiaji upo huru kuchangia mawazo yako kwa mada tutakazokuwa tunaziweka hapa.